RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amesema, tozo zitakazotozwa katika miamala ya simu Septemba na Oktoba 2021, zitakwenda kujenga vyumba vya madarasa zaidi ya 500 nchi nzima. Anaripoti Vicktoria Mwakisimba, TUDARCo…(endelea).
Tozo hizo zilianza kutozwa tarehe 15 Julai 2021 ambapo hadi kufikia 30 Agosti 2021, zaidi ya Sh.60 bilioni zilikuwa zimekusanywa na kupelekwa kujenga miradi ya sekta ya afya.
Akizungumza na wananchi wa Tegeta, mkoani Dar es Salaam akiwa njiani kwenda Bagamoyo Mkoa wa Pwani, leo asubuhi Alhamisi, tarehe 2 Septemba 2021, Rais Samia amesema, lengo ya tozo hizo ni kutekeleza miradi ya maendeleo.
“Miradi ya maendeleo, tutaimaliza kama tulivyopanga na nataka kuwahakikishi, tutakwenda kuitekeleza kama tulivyopanga na huko nyuma tulikuwa tunaitekeleza tukipata misaada, lakini sasa tunaitekeleza kwa fedha zetu,” amesema Rais Samia
“Tuliweka tozo kwenye mambo ya fedha za mitandao, yamepigiwa kelele sana, nimesikia na tumekaa na wataalamu na kupunguza asilimia 30, nataka kuwaeleza tozo zitaendelea kuwepo na wala sitawaficha,” amesema .
Amesema, toka tumeanza kutekeleza tumekusanya zaidi ya bilioni 60 na tunatekeleza miradi yetu sisi wenyewe na kama mnavyojua, Januari tuna wimbi kubwa la watoto wanaotaka kuingia darasa la kwanza.
“Fedha tutakazozikusanya mwezi huu wa Septemba na Oktoba, tunakwenda kujenga madarasa zaidi ya 500 nchi nzima,” amesema
Kuhusu ombi la Mbunge wa Kawe, Askofu Josephat Gwajima la kujengwa kwa shule, Rais Samia amesema “Shule iliyoombwa hapa itakwenda kujenga na kitakachokusanywa miezi miwili ijayo, itakwenda kujenga.”
“Sasa wanadamu ukifanya watasema na usipofanya watasema, bora tufanye waseme wakione kuliko kutokufanya wakasema,” amesema huku akisisitiza
“misaada siku hizi ni michache sana, lazima tuminyane sisi wenyewe.”
Kuhusu safari yake hiyo ya Bagamoyo amesema “unakwenda katika vivutio mbalimbali, tunakwenda kuitangaza Tanzania ulimwenguni na tutakwenda kuizindua filamu yetu Marekani na itafungua milango ya kuitangaza zaidi Tanzania na itatuonyesha tunavyoishi, tulivyo, siasa zetu na wanaopeleka uongo utafahamika.”
Asante kwa kutuhabarisha. Nawatakia kazi njema mno.
Rafiki yako,
Aliko Musa.
Mbobezi Kwenye Ardhi Na Majengo