SAMIA Suluhu Hassan, Rais wa Tanzania, amewaomba viongozi wa dini nchini humo, kutokutumia nafasi zao kufanya siasa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Morogoro…(endelea).
Rais Samia ametoa nasaha hizo, leo Alhamisi, tarehe 8 Julai 2021, wakati akizungumza katika Mkutano Mkuu wa 31 wa Jumuiya ya Kikristo Tanzania (CCT), unaofanyika Kilakala, Mkoa wa Morogoro.
Amesema, viongozi wa dini wana nafasi kubwa katika jamii kwani wanayoyasema yabaki mioyoni mwa waumini wao tofauti na yale yanayosemwa na wanasiasa.
“Wakati mwingine dini na siasa ni vitu vinakwenda sambamba na wakati mwingine vinakinzana, inategemea mtu anaitumiaje, lakini kuna ubaya unapoitumia dini ile kufanya siasa,” amesema Rais Samia
Aidha, ametumia fursa hiyo, kuwaomba viongozi wa dini, kuhakikisha wanatumia nafasi yao kuwasisitiza waumini kuendelea kuchukua tahadhari ya maambukizi ya virusi vya corona (COVID-19).
“Nawaomba maaskofu na viongozi wengine wa dini, kuendelea kuwakumbusha waumini wenu kuendelea kuwasisitiza umuhimu wa kujikinga na corona,” amesema Rais Samia
Leave a comment