RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amesema atafanya mazungunzo na vyama vya siasa ambavyo havishiriki katika masuala mbalimbali ya kuamua mustakabali wa kisiasa nchini, ili ajue wanataka nini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Jumatatu, tarehe 21 Machi 2022, Ikulu jijini Dar es Salaam, akipokea taarifa ya awali ya utendaji wa kikosi kazi cha kuratibu maoni ya wadau wa demokrasia ya vyama vingi vya siasa.
Kiongozi huyo wa Tanzania, amesema lengo la uamuzi huo ni kuhakikisha vyama vyote vinakuwa kitu kimoja katika uendeshaji wa siasa zenye tija.
“Najua kwamba kwenye vyama vya siasa hamjakaa vizuri sana, bado kuna vyama vya siasa ushiriki wao una…lakini nitaendelea ku-engage nao, kukaa na kuzungumza nao niwasikilize na nione wanataka maboresho yepi,” amesema Rais Samia na kuongeza:
“Tuwafanyie nini? Lengo ni wote twende kwenye treni moja, sio wengine wako kwenye treni, wengine wako nje, hapana. Wote tuingie kwenye treni tuendeshe siasa zenye tija kwenye Taifa letu.”
Miongoni mwa vyama vya siasa ambavyo havijashiriki mikutano ya wadau wa tasnia hiyo inayoitishwa kujadili mambo mbalimbali ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), ambacho kilikataa kushiriki mkutano uliotishwa na Baraza la Vyama vya Siasa, na kufanyika jijini Dodoma mwishoni mwa 2021.
Chadema kiligoma kushiriki mkutano huo wa wadau wa vyama siasa, uliokuwa chanzo cha uundwaji wa kikosi kazi hicho na kutaja sababu mbalimbali zilizosababisha kuchukua hatua hiyo, ikiwemo Mwenyekiti wake, Freeman Mbowe, kuwa mahabusu akikabiliwa na mashtaka ya ugaidi.
Licha ya Mbowe kuachwa huru, bado Chadema kimegoma kushiriki kongamano la haki, lililoandaliwa na Kituo cha Demokrasia nchini (TCD), linalotarajiwa kufanyika jijini Dodoma mwishoni mwa Machi 2022, kikidai halina nia ya kujadili upatikanaji wa katiba mpya.
Hongera Mama!
Umeonyesha kwamba “Kusikiliza Siyo Udhaifu wa Kuongoza.”