RAIS Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuzindua Tamasha la Kwanza la Michezo la Wanawake la Tanzanite litakalofanyika katika viwanja vya Uhuru na Benjamin Mkapa jijini Dar es salaam kuanzia tarehe 16 hadi 18 Septemba, 2021 huku uzinduzi rasmi ukifanyika Jumamosi, tarehe 18 Septemba. Anaripoti Victoria Mwakisimba TUDARCo … (endelea).
Katibu Mkuu anayesimamia sekta za sanaa, utamaduni na michezo, Dk.Hassan Abbasi ameyasema hayo jana tarehe 15 Septemba, 2021 alipozungumza na waandishi wa habari kwenye Uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam.
“Toka aingie madarakani Rais Samia ameonesha nia ya dhati ya kuinua michezo kwa wanawake hivyo amekubali kuja kuzindua tamasha hili ambalo litaanza tarehe 16-18 Septemba, 2021” amefafanua Dk. Abbasi.
Amesema tamasha hilo la kihistoria limesheheni michezo mbalimbali ikiwemo riadha, ndondi, soka, netiboli, mpira wa kikapu, wavu, karate, makomando wa kike, kuvuta kamba, rede na mingine mingi.
“Katika kunogesha tamasha hilo kutakuwepo wasanii mbalimbali wa muziki wa kizazi kipya huku asilimia zaidi ya 98 wakiwa ni wa kike ambao nao wataonesha uwezo wao,” alisema Dk. Abbasi.
Leave a comment