RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan leo Jumapili tarehe 28 Machi 2021, atapokea taarifa ya Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) ya mwaka 2019/20. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Pia, atapokea taarifa ya Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) zote za mwaka 2019/20.
Taarifa iliyotolewa jana Jumamosi na Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu imesema, hafla hiyo, itafanyika Ikulu, Chamwino mkoani Dodoma kuanzia saa 4:00 asubuhi.
Hii itakuwa hafla ya kwanza kwa Rais Samia kuifanya tangu alipoingia madarakani tarehe 19 Machi 2021, akipokea kijiti kilichoachwa wazi na aliyekuwa Rais Dk. John Pombe Magufuli.
Kabla ya kuapishwa kuwa Rais, Samia alikuwa makamu wa Rais wa Tanzania, tangu 5 Novemba 2015, akimsaidia Dk. Magufuli.
Dk. Magufuli alifariki dunia Jumatano ya tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Dar es Salaam na mwili wake kuzikwa Ijumaa 26 Machi 2021, nyumbani kwao Chato mkoani Geita.
Leave a comment