RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameahidi kufanya marekebisho kadhaa katika sera na sheria sambamba na kuondoa vikwazo katika kukuza uwekezaji. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Akihutubia Bunge kwa mara ya kwanza tangu aapishwe kushika mamlaka ya juu ya nchi leo tarehe 22 Aprili 2021, Rais Samia amesema, serikali yake itaendelea kuboresha sera za fedha ili kudhibiti sarafu ya Tanzania.
“Tutafanya marekebisho kadhaa katika sera, sheria na kuondoa vifungu vitakavyokuwa vikwazo katika kukuza uwekezaji.
“Tutaendelea kuboresha sera za fedha kuhakikisha viashiria vyote vya uchumi kama mfumuko wa bei unadhibitiwa, sambamba na kukuza thamani ya sarafu,” amesema.
Amesema, kwa sasa kumekuwa na mzunguko mkubwa kwa wawekezaji pale wanapotaka kuwekeza, na kwamba Serikali ya Awamu ya Sita inataka uwekezaji wa haraka.
“Ndani ya nchi yetu, kumekuwa na mizunguko mikubwa watu wanapokuja kwa ajili ya uwekezaji, Serikali ya Awamu ya Sita tunakwenda kukomesha hilo na uwekezaji utakwenda kufanyika kwa haraka,” amesema.
Leave a comment