RAIS wa Awamu ya Sita, Samia Suluhu Hassan, amesema anapanga kukutana na viongozi wa vyama vya siasa, ili kujadili namna ya kuiendesha nchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Rais Samia amesema hayo leo Alhamisi tarehe 22 Aprili 2021, akihutubia Bunge, jijini Dodoma.
Kiongozi huyo amesema, katika mkutano huo, yeye pamoja na viongozi wa vyama vya siasa, watajadili namna ya kuweka muelekeo wa kuendesha shughuli za kisiasa zenye tija kwa Taifa.
“Katika kulinda uhuru wa demokrasia, nakusudia kukutana na viongozi wa vyama vya siasa ili kwa pamoja tuweke muelekeo wa kuendesha shughuli za kisiasa zenye tija na maslahi kwa nchi yetu,” amesema Rais Samia.
Rais Samia aliyeapishwa tarehe 19 Machi 2021, kurithi mikoba ya aliyekuwa Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dk. John Magufuli, amesema hayo wakati akitoa muelekeo wa serikali yake ya Awamu ya Sita katika kuimarisha demokrasia, uhuru wa watu na vyombo vya habari.
“Maeneo mengine yatakayofanyiwa kazi na serikali ni pamoja na kulinda misingi ya kidemokrasia na uhuru wa watu pamoja na vyombo vya habari, kama mnavyofahamu uhuru na demokrasia ni msingi wa amani katika nchi na pia vinasaidia kuchochea maendeleo ya kisiasa, kiuchumi na kijamii,” amesema Rais Samia.
Hata hivyo, amewataka Watanzania kufuata sheria na taratibu za nchi katika kazi za siasa.
“Hata hivyo, naomba niseme kuwa hakuna uhuru wa demokrasia unaosimamiwa na kulindwa na Katiba, sheria, taratibu na kanuni. Hivyo basi, pamoja na demokrasia na uhuru wa watu, niwaombe Watanzania tujidhatiti kufanya kazi zetu kwa kuzingatia sheria za nchi yetu,” amesema Rais Samia.
Leave a comment