RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan atahutubia Bunge la nchi hiyo, Alhamisi jioni ya tarehe 22 Aprili 2021. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Leo asubuhi Jumatatu, tarehe 19 Aprili 2021, Spika wa Bunge, Job Ndugai amewatangazia wabunge kuwa, Rais Samia atalihutubia bunge hilo.
Kiongozi huyo wa Bunge, amewataka wabunge wote walioko nje ya Dodoma kuhakikisha wanarejea jijini humo na kwamba, wale walio na ratiba za kuondoka, wasifanye hivyo hadi shughuli hiyo itakapokwisha.
Rais Samia atalihutubia Bunge kwa mara ya kwanza, tangu alipoingia madarakani tarehe 19 Machi 2021, akichukua nafasi ya iliyoachwa wazi na Dk. John Magufuli.
Dk. Magufuli alifariki dunia jioni ya tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Dar es Salaam, mwili wake ulizikwa Ijumaa ya tarehe 26 Aprili 2021, nyumbani kwao, Chato mkoni Geita.

Bunge hilo la 12, lilizinduliwa na Hayati Magufuli tarehe 13 Novemba 2020, kwa mujibu wa Ibara ya 91(1) ya Katiba ya Tanzania inayoeleza “Rais atalihurubia Bunge jipya katika mkutano wake wa kwanza na kulifungua rasmi bunge hilo.
Kwa kuwa Bunge hilo limekwisha zinduliwa, Rais Samia anakwenda kulihutubia kwa mujibu wa Ibara ya 91 (2) inayoeleza “bila ya kuathiri masharti ya ibara ndogo ya (1); Rais aweza wakati wowote kulihutubia Bunge au kupeleka kwenye Bunge taarifa ambayo itasomwa na Waziri.”
Rais Samia anakwenda kuhutubia bunge hilo kipindi wakati ambao chombo hicho cha kutunga sheria ‘kikitawaliwa’ na wabunge wengi kutoka chama anachotoka yeye – Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Bunge hilo kwa sasa limezama katika Pia mjadala mkali kwa wanaotetea utumishi wa Hayati Magufuli na ule wa sasa wa Rais Samia.
Kutokana na mvutano huo mkali, jana Jumapili, katika kongamano la kuombea taifa na kumshukuru Mungu kwa maisha ya hayati Magufuli, Rais Samia aliwaonya wabunge hao na kuwataka kujikita kujadili bajeti.
“Inasikitisha sana, watu wanapiga ngoma mitandaoni ila watu wanacheza bungeni, tena wana demka kweli. Mnalinganisha Magufuli na Samia, hawa watu ni kitu kimoja, nimekuwa nafuatilia mijadala bungeni, haina afya kwa taifa letu,” amesema Rais Samia.
“Naomba sana, kipindi hiki wabunge, tunatakiwa kupitisha bajeti za sekta mbalimbali na mjikite sana huko na mengine tutayazungumza siku zinavyokwenda. Tufanye kazi kama Bunge linavyotakiwa kufanya kazi,” alisema Rais Samia.
Pia, hotuba hiyo ya Rais Samia, ataitoa ikiwa imesalia takribani wiki moja, kabla ya kufanyika kwa mkutano mkuu maalum wa CCM, wenye agenda kuu moja ya kumthibitisha kuwa mwenyekiti wa chama hicho.
Leave a comment