SERIKALI ya awamu ya sita nchini Tanzania inayoongozwa na Rais Samia Suluhu Hassan imedhamiria kundeleza kilimo cha mazao ya chakula na biashara. Anaripoti Helena Mkonyi, TUDARCo … (endelea).
Hayo yamesemwa leo Alhamisi, tarehe 16 Septemba 2021 na Waziri Mkuu wa Tanzania, Kassim Majaliwa kwa niaba ya Rais Samia, wakati akiwa ziarani mkoa wa Kigoma.
Majaliwa alikuwa akikagua shamba la michikichi katika kambi ya Jeshi la Kujenga Taifa (JKT) 821 KJ, Bulombora mkoani humo.
Amesema “Serikali inafuatilia kwa ukaribu kilimo cha mazao hayo likiwemo zao la mchikichi.”
Majaliwa amewataka wazazi kuwaanzishia watoto wao mashamba ya michikichi kwa ajili ya kuwakwamua kiuchumi na kuwaepusha watoto wao kuwa tegemezi.
Pia amewaomba wananchi wote waliopo katika mikoa inayolima zao hilo wajihusishe katika kulima zao hilo kwa ajili ya kukuza pato la Taifa.
“Wekezeni katika kilimo cha mchikichi kwa ajili ya maendeleo yenu na ya watoto wenu,” amesema Majaliwa
Amesema, Serikali imeamua kulipa kipaumbele zao hilo ili kumaliza tatizo la upungufu wa mafuta ya kula nchini Tanzania kwani serikali inatumia zaidi ya Sh.400 billioni kwa mwaka kuagiza mafuta nje ya nchi.
Aidha, Majaliwa amelipongeza Jeshi la Kujenga Taifa na kambi yake ya Bulombora kwa kuitikia wito wa kulima zao la michikichi kwa vitendo na kwamba shamba hilo linatarajiwa kuwa la mfano kwa kilimo cha mchikichi.
Kwa upande wake, Mkuu wa Jeshi la Kujenga Taifa, Meja Jenerali Rajabu Mabele amesema kambi hiyo wamepanga kupanda ekari 2,000 za michikichi kwa awamu, ambapo mwaka jana walipanda ekari 500 na mwaka huu wanatarajia kupanda eneo jingine la ukubwa wa ekari 500.
Leave a comment