RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewahakikishia mazingira mazuri wafanyabiashara wa Kenya na Tanzania, akisema upande mmoja kuna uhuru wa kufanyabiashara na mwingine kuna suluhu ya kuondosha vikwazo vya biashara. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Samia ameyasema hayo leo Jumatano, tarehe 5 Mei 2021, katika Jukwaa la Wafanyabiashara wa Kenya na Tanzania, lililofanyika jijini Nairobi nchini Kenya.
Ni siku ya pili ya ziara yake nchini humo aliyoianza jana Jumanne kwa mwaliko wa Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta.
Akihitimisha hotuba yake, Rais Samia amesema “mna bahati kwamba, nchi zetu mbili, upande mmoja kuna uhuru wa kufanya biashara na upande mwingine kuna suluhu ya kuondosha vikwazo vya biashara. Kwa hiyo mshindwe ninyi.”
Msemo huo wa Rais Samia unatokana na majina ya viongozi wa mataifa hayo, ambapo yeye binafsi jina lake la kati ni Suluhu, huku Rais wa Kenya, akiitwa Uhuru Kenyatta.
Akizungumzia jukwaa hilo, Rais Samia amesema, anaimani litakuwa mwanzo wa kumaliza changamoto za wafanyabishara kati ya Kenya na Tanzania pamoja na Ukanda wa Afrika Mashariki.
“Ni matumani yangu jukwaa hii ni mwanzo wa kumaliza changamoto zenu, Tanzania iko tayari kupokea jumuiya za wafanyabiashara kutoka Kenya, tuko tayari kuwakumbatia na kushirikiana. Serikali yangu iko zaidi ya tayari kutoa ushirikiano baina ya wafanyabiashara wa pande zote mbili,” amesema Rais Samia.
Kiongozi huyo wa Tanzania amesema, Serikali yake iko tayari kupokea mapendekezo yatakayotolewa katika jukwaa hilo kuhusiana na changamoto zilizopo kwa wafanyabiashara wa pande zote mbili.
“Tunajua viwango vyetu vya biashara sio vizuri, naamini jukwa hili ni fursa ya wafanyabiashara kuwasiliana na kueleza mikakati ya kuimarisha biashara na kuondoa umasikini kwa wananchi wetu,” amesema Samia.
Akielezea mikakati yake ya kuboresha sekta binafsi hasa katika masuala ya uwekezaji na biashara, Rais Samia amesema, serikali yake imejidhatiti kuiwezesha sekta hiyo kukabiliana na changamoto za uchumi wa kidunia.
“Tanzania imejidhatiti kuona sekta binafsi ina uwezo wa kukabiliana na changamoto za uchumi wa kidunia kupitia kwenye sera zetu za viwanda. Tunaamini viwanda ndio msingi wa uongezaji thamani bidhaa zetu ambazo zinatengeneza ajira kwa wananchi,” amesema Rais Samia na kuongeza.
“Kwa sasa tunachukua hatua mbalimbali kuboresha mazingira ya ufanyaji biashara, kama kufanya mapitio kwenye masuala ya ushuru na yasiyo ya ushuru katika biashara, kuanzisha kituo kimoja cha uwekezaji, kuondoa kodi kandamizi, Kupambana na rushwa katika sekta binafsi,” amesema
Leave a comment