RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ameyataka Mashirika Yasiyo ya Kiserikali (NGO’s) na Asasi za Kiraia nchini, kufanya utetezi wa haki za binadamu kwa kuzingatia misingi ya katiba, sheria, mila na tamaduni za nchi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Maagizo hayo ya Rais Samia yametolewa leo Alhamisi, tarehe 12 Mei 2022 na Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Damas Ndumbaro, akifungua kikao kazi cha kupitisha mpango mkakati wa Asasi za Kiraia kuhusu utekelezaji wa mapendekezo 167 yaliyokubaliwa na Tanzania kwenye duru la tatu la Mchakato wa Tathimini ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa (UPR).
“Rais Samia naye amenipa ujumbe niwafikishie kwa siku ya leo, Rais ameagiza niwaleze kwamba Serikali yake itaendelea kushirikiana na sasi zote zinazohusiana na masuala ya haki za binadamu.
Ameniagiza niwapongeze kwa kazi nzuri mnayofanya ya kuendelea kusimamia kutetea haki za binadamu,” amesema Dk. Ndumbaro.
Dk. Ndumbaro amesema “Rais ameniomba muendelee kumsaidia yeye, Serikali katika kulinda na kuendeleza haki za binadamu kwa kuzingatia na kuimarisha amani na utulivu, anasisitiza sana Utanzania wetu sababu haki za binadanu lazima ziwe kwenye katiba na sheria zetu.”
Aidha, Dk. Ndumbaro amezishauri Asasi za Kiraia kutumia kipindi hiki cha uongozi wa Rais Samia, kuimarisha hali ya utetezi za haki za binadamu kwa kuwa ni muumini wa suala hilo.
“Na mimi nikiangalia wazi utawala wa Awamu ya Sita utafuja mwaka 2030 na sisi Watetezi wa Haki za Binadamu tunatakiwa kuutumia sababu Rais Samia ni mwenzetu lazima tutumie fursa hii kuweka hoja zetu ili zisikike sana na tumuunge mkono,” amesema Dk. Ndumbaro.
Leave a comment