RAIS Samia Suluhu Hassan, amewataka wananchi wazoee tozo zinazotozwa katika baadhi ya huduma za usafirishaji, kwa kuwa barabara za kulipiwa zitajengwa nyingi nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Ijumaa tarehe 11 Novemba, 2022, katika hafla ya uzinduzi wa mradi wa maji Kigamboni, baada ya Mbunge wa jimbo hilo, Dk. Faustine Ndugulile, kumuomba aondoe tozo inayotozwa kwa wananchi wanaopita katika Daraja la Kigambo, ili kuwaondolea mzigo wa malipo hayo.
“Nataka niseme wananchi mzoee barabara za aina hii zitakuja nyingi katika nchi yetu. Ile kitu bure kidogo kidogo itaondoka, ili tuendelee lazima tuwe na barabara, madaraja makubwa, vivuko vizuri na hayo yataletwa na sekta binafsi. Ili sekta binafsi waendelee lazima wananchi tulipie huduma,” amesema Rais Samia.
Mkuu huyo wa nchi amemjibu Dk. Ndugulile akisema tozo hizo haziwezi kuondolewa kwa kuwa daraja hilo limejengwa kwa mkopo ambao unatakiwa urudishwe, bali Serikali itaendelea kuangalia namna ya kuipunguza.
“Daraja la Kigambo ni mkopo lazima turudishe na hakuna wa kurudisha isipokuwa wananchi wenyewe wanaopata huduma. Ni uzoefu wa mwanzo kuona wananchi wanalipa kupita pale, wengine walisema mbona daraja Tanzanite watu hawalipishwi, Tanzanite ni fedha ya Serikali asilimia 100, Kigamboni ni mkopo lazima urudishwe,” amesema Rais Samia.
Leave a comment