RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewataka wananchi kupaza sauti zao wanapokutana na changamoto za huduma ya afya, ili Serikali yake izifanyie kazi. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Kiongozi huyo wa Tanzania, ametoa wito huo leo Jumanne tarehe 1 Juni 2021, alipofanya ziara ya kushtukiza katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Mwananyamala, mkoani Dar es Salaam.
Rais Samia alitoa kauli hiyo baada ya kugawa mashuka 200, katika hospitali hiyo.
“Hospitali iko vizuri na mimi nimetoa zawadi kidogo ya mashuka 200, ili wagonjwa wetu walale vizuri. Sasa mkikuta mashuka yamechanika chanika, wagonjwa wamelazwa, pigeni kelele tusikie. Sababu mashuka 200 si haba,” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia amesema Serikali yake inaendelea kutatua changamoto zinazoikabili sekta ya afya nchini, ikiwemo upungufu wa dawa na vifaa tiba.
“ Lakini nitaenda kwenye hospitali nyingine kurekebisha mambo, nimesikia upungufu wa dawa jambo ambalo nakwenda kulifanyia kazi. Kuna mambo machache hayajakamilika, tunaenda kukamilisha,” amesema Rais Samia.
Leave a comment