RAIS Samia Suluhu Hassan, ameipongeza timu ya madaktari na wauguzi wa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, waliofanikisha upasuaji wa kuwatenganisha mapacha waliokuwa wameungana, Rehema na Neema, huku akiwaombea watoto hao wapone haraka. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Rais Samia ametoa pongezi hizo leo Jumamosi, tarehe 2 Julai 2022, kupitia ukurasa wake wa Twitter, siku moja baada ya madaktari hao kufanya upasuaji.
“Nawapongeza madaktari na wauguzi wa Hospitali ya Taifa Muhimbili, kwa kufanikisha upasuaji wa kuwatenganisha watoto mapacha walioungana. Hii ni hatua muhimu katika utekelezaji wa mpango wa serikali kuboresha matibabu ya kibingwa. Nawaombea watoto Rehema na Neema wapone haraka,” ameandika Rais Samia.
Watoto hao mapacha, walikuwa wameungana sehemu ya kifua, tumbo na ini, ambapo walifanyiwa upasuaji kwa muda wa zaidi ya saa sita.
Kwa mujibu wa Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Watoto katika hospitali hiyo, Dk. Zaitun Bokhari, amesema upasuaji wa mapacha hao ulifanywa na madaktari 12, ambao ni madaktari wa usingizi sita, wa kutenganisha ngozi wane, wa kuangalia mfumo wa watoto kama unakwenda vizuri wawili na wauguzi sita.
Leave a comment