RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewaomba wanawake wamuunge mkono katika uongozi wake, ili alifikishe Taifa sehemu nzuri. Anaripoti Jemima Samwel, DMC … (endelea).
Wito huo ameutoa leo Jumanne, tarehe 8 Juni 2021, akizungumza na wanawake wa Mkoa wa Dodoma.
Rais Samia amesema wanawake ndio wajenzi wa Tanzania, kutokana na idadi yao kuwa kubwa nchini ikilinganishwa na wanaume, lakini pia mwanamke hashindwi na kitu.
“Mwanamke ni msimamizi wa sheria na tuna anza nyumbani, sisi ndiyo wajenzi wa Tanzania yetu. Twendeni tukasimamie, niungeni mkono nisaidieni. Kufika hapa ndugu zangu ni changamoto kubwa, nisaidieni, tulifikishe hili Taifa linapostahili kuwa,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amewataka wanawake waliofanikiwa katika sekta mbalimbali, ikiwemo viongozi na watendaji wa taasisi binafsi na za Serikali, kuwashika mkono wanawake wenzao katika kujitafutia maendeleo.
“Niwahimize wanawake wenzangu mliobahatika kupata nafasi za uongozi, mjitahidi kuwa chachu kwa wanawake wengine wanaotuangalia kama mifano yao. Sisi tulioshika nafasi mbalimbali tujioneshe mfano mzuri, wanaotufuata nyuma watake kutuiga wafike tunakotaka kufika sisi,” amesema Rais Samia.
Licha ya wito huo, Rais Samia amewataka wanawake wawe mabalozi wazuri katika kupinga vitendo vya uharibifu wa mazingira, kwani vinasabisha madhara makubwa, ikiwemo kukauka kwa vyanzo vya maji.
“Maeneo mengi tunayofahamu kuwa na vyanzo vya maji, sasa vyanzo vimekauka ndiyo maana tunapata shida kupeleka maji vijijini. Vyanzo tunavyofahamu havipo, inabidi tutoe vyanzo vikuu tusambaze maji jambo ambalo linachukua fedha nyingi,” amesema Rais Samia.

Hali kadhalika, Rais Samia amewataka wanawake kusimamia usafi wa mazingira yao.
“Niwaambie Watanzania tulitelekeza kutunza mazingira ya aina yote, vijijini kutunza miti na hewa zetu na mazingira ya usafi mijini,”
“ Katika mabaraza yetu tuna wanawake, uchafu tunaouona njiani unazagaa madiwani wanawake tupo. Lakini tunaluka uchafu, twendeni kujiunga kama sisi kwa kusema uchafu unaondoka kwenye nchi yetu,” amesema Rais Samia.
Aidha, Rais Samia amewataka wanawake wasihahau majukumu yao katika utunzaji familia akisema “tusisahau majukuimu yetu ya kulea familia kiujumla, mwanamke ni mzazi na mama mlezi wa watoto na baba wao watoto, mwanamke ni mwalimu wa familia.”
Leave a comment