RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amewahakikishia wafanyabiashara wa China kuandaa mazingira mazuri ya biashara nchini. Anaripoti Nasra Bakari, DMC … (endelea).
Ametoa kauli hiyo leo tarehe 21 Aprili 2021 alipokutana na viongozi wa Jumuiya ya Wafanyabiashara wa China nchini Tanzania (Chinese Business Chamber of Tanzania), na kuzungumzumza nao kuhusu masuala mbalimbali yanayohusu biashara na uwekezaji.
Janson Huang akiongoza wafanyabiashara wenzake, amempa pole Rais Samia kufuatia msiba kitaifa wa kuondokewa na aliyekuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Hayati John Magufuli.
Wafanyabiashara hao wamemhakikishia Rais Samia kwamba, China wapo tayari kushirikiana na serikali yake katika kukuza uchumi na kuinua ustawi wa wananchi, kupitia uwekezaji mkubwa wanaokusudia kuufanya kupitia kampuni zaidi ya 800 za China zilizotayari kuwekeza Tanzania.
Viongozi hao wametaja maeneo ambayo kampuni zao zipo tayari kuwekeza kuwa ni viwanda vya kutengeneza simu, dawa za binadamu, magari, kuanzisha maeneo maalum ya viwanda (Industrial Parks) na kuwawezesha Watanzania kupata ujuzi kupitia mpango wa elimu utakaotoa fursa kwa Watanzania kusoma vyuo vya Tanzania na China.
Akizungumza na viongozi hao, Rais Samia amewashukuru kwa salamu zao za pole na pongezi, amewahakikishia kuwa serikali yake itashirikiana nao katika uwekezaji.
Na kwamba, itaboresha zaidi mazingira ya biashara na uwekezaji ili matokeo ya uwekezaji huo yanufaishe pande zote mbili.
Leave a comment