RAIS Samia Suluhu Hassan amesema atawapima Waziri wa Sanaa, Michezo na Utamaduni, Inocent Bashungwa pamoja na naibu wake, Pauline Gekul kwa kuwa kufuatiliana namna watakavyopandisha timu za Taifa na kukuza michezo mbalimbali nchini. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo tarehe 27 Oktoba mwaka huu, Ikulu jijini Dar es Salaam katika hafla ya kuipongeza Timu ya taifa ya wanawake ya Tanzania – Twiga Stars kwa kutwaa ubingwa wa kombe la COSAFA mapema mwezi huu.
Amesema sekta za utamaduni, sanaa na michezo zinatakiwa kupewa kipaumbele kwa sababu ni sekta zinazozalisha ajira kwa vijana wengi.
“Hivyo tambueni kwamba nitawapima kupitia kipimo hiki, jinsi mtakavyopandisha timu na kukuza michezo ndivyo nitakavyojua mnafanya kazi zenu vizuri,” amesema Rais Samia.
Amesema hivi karibuni alifanya mabadiliko ya wizara, baina ya habari na wizara ya sanaa, michezo na utamaduni.
“Nilifanya hivyo kuitoa habari na kuipeleka kule inakohusika zaidi ili viongozi wa wizara hii wajielekeze zaidi kwenye michezo, sanaa na utamaduni wetu,
“Nimpongeze waziri na naibu wake kwa kuendelea kupata imani kunisaidia katika jukumu hili kubwa, najua katika kipindi hiki cha mpito mlipokuwa hamjijui roho zilikuwa juujuu lakini juzi mlipata ithibati ya kuendelea kufanya kazi hii nami nawataka mkachape kazi,” amesema Rais Samia.
Amesemsema Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2020- 2025 pamoja na mambo mengine imeelekeza kwamba sekta za utamaduni, sanaa na michezo zipewe kipaumbele jambo ambalo linatakiwa kuzingatiwa na mawaziri hao.
Leave a comment