RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amefanya mazungumzo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Royal Dutch Shell, Ben Van Beurden, kuhusu masuala ya uwekezaji katika mradi wa gesi asilia iliyosindikwa (LNG). Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia amefanya mazungumzo hayo leo Jumatatu, tarehe 4 Oktoba 2021, kwa njia ya mtandao, Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma, na kuhudhuriwa na Waziri wa Nishati, January Makamba na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Mbarouk Nassor.
Wengine walioshiriki ni, Katibu Mkuu Wizara ya Nishati Mhandisi Leonard Masanja na Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Dk. James Mataragio.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais- Ikulu, Jaffar Haniu, Rais Samia amemshukuru Van Beurden, kwa nia yao njema ya kutaka kuwekeza kwenye mradi huo, ambao utachochea kukuza uchumi wa Tanzania.
“Rais Samia leo tarehe 04 Oktoba, 2021 amezungumza kwa njia ya mtandao na Ben Van Beurden, Afisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Royal Dutch Shell yenye makao yake makuu nchini Uholanzi,” imesema taarifa ya Haniu.
Kwa upande wake, Van Beurden amesema wanarishishwa na namna Serikali ya Rais Samia, ilivyoboresha mazingira ya uwekezaji katika mradi huo.
“Van Beurden amemshukuru Rais Samia na kueleza kuwa, wanaridhishwa na jinsi Serikali ya Awamu ya Sita, ilivyoboresha mazungumzo ya uwekezaji kwenye mradi wa Gesi asili iliyosindikwa (LNG) hapa nchini,” imesema taarifa ya Haniu.
Leave a comment