RAIS wa Tanzania Samia Suluhu Hassan amefurahishwa na uwepo wa vyumba vya faragha vya wajawazito kujifungulia wakiwa na wenza wao katika jengo la mama na mtoto kwenye Hospitali ya CCBRT jijini Dar es Salaam. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mkuu huyo wa nchi ametaka vyumba hivyo pia viwepo katika hospitali za umma ili kusaidia kubadilisha baadhi ya mienendo ya wanaume ikiwemo kuzingatia uzazi wa mpango na kuhudumia vizuri wajawazito.
Rais Samia ameyasema hayo leo Jumanne tarehe 5 Julai, 2022 wakati wa uzinduzi wa jengo la mama na mtoto katika Hospitali hiyo ambalo limepewa jina la Samia Suluhu Hassan.
“Lazima wale wajamaa tuingie nao huko ili wakaone kinachotokea,” amesema Rais Samia nakuongeza;
“Wanaume zetu wakiona kishindo tunachopambana nacho kule ndani na kwa maana hiyo watasaidia kwenda kwenye uzazi wa mpangilio lakini sio hilo tu watajitahidi watoe huduma ya kutosha ili siku ile ikifika mama awe na njia nyepesi ya kuleta kiumbe duniani.”
Mbali na huduma hiyo Samia amesema pia amefurahia huduma kwa watu wenye ulemavu na mabinti wadogo waliopata mimba za utotoni na wale wenye tatizo la fistula.
Amesema jambo jingine lilomfurahisha ni hospitali kufanya uchunguzi wa mapema ya watoto wanaozaliwa na ulemavu kama mdomo sungura, mguu kifundo kabla hawajapata madhara makubwa zaidi.
“Huduma zote hizi zinafanya hospitali hii kuwa ya kisasa hapa nchini na kwamaana hiyo wala sijuti hospitali hii kupewa jina langu,” amesema Rais Samia.
Tayari watoto 65 wamezaliwa katika hospitali hiyo tangu kuanza kutoa huduma tarehe 3 Januari 2022 na kati ya hao familia tatu zilipata mapacha na kina mama wawili walikuwa wenye ulemavu na wote walitoka wakiwa na hali nzuri.
Leave a comment