Rais Samia Suluhu Hassan amesisitiza uharakishwaji wa mchakato wa matumizi ya lugha ya Kiswahili kupitishwa rasmi kama lugha ya nne itakayotumika katika nchi za ukanda wa Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC). Anaripoti Erick Mbawala, TUDARCo … (endelea).
Pia amesisitiza umuhimu wa usalama wa chakula katika ukanda mzima wa SADC na kuzisihi nchi hizo kuwekeza kwenye ‘uchumi wa buluu’.
Rais Samia ametoa mapendekezo hayo jana tarehe 17 Agosti, 2022 katika mkutano wa 42 wa SADC uliofanyika jijini Kinshasa – Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Katika mkutano huo uliopitisha mazimio 27, Rais Samia alitoa maoni yake kwa lugha ya Kiswahili kama namna ya kuchapusha matumizi ya lugha hiyo kuwa miongoni mwa nchi Wanachama wa SADC.
Aidha, akizungumzia uwiano wa kijinsia waliokubaliana katika ukanda huo, Rais Samia amesema Tanzania imejitahidi kutoa fursa kwa wanawake hasa katika nafasi za uongozi za kimkakati.
Miongoni mwa nafasi hizo za uongozi serikalini na bungeni ni pamoja na uwaziri wa ulinzi, mambo ya nje, uwekezaji, utalii pamoja na nafasi ya Spika wa Bunge.
Mkutano huo wa SADC pia ulishuhudia makabidhiano ya Uenyekiti kutoka kwa Rais wa Malawi, Dk. Lazarus Chakwera na sasa nafasi hiyo imechukuliwa na Rais wa DRC, Felix Tshisekedi.
Rais Samia leo atafanya ziara ya kikazi uya siku moja nchini DRC ambapo pamoja na mambo mengine, atafanya mazungumzoa na mwenyekiti wake, Rais Felix Tshisekedi.
Leave a comment