RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametoa msamaha kwa wafungwa 5,704, katika kuadhimisha miaka 60 ya Uhuru wa Tanzania Bara. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Jumatatu, tarehe 27 Desemba 2021 na Waziri wa Mambo ya Ndani, George Simbachawene, akizungumza na wanahabari jijini Dar es Salaam.
“Rais Samia kwa kutumia madaraka aliyopewa chini ya Ibara ya 45 (1) (d) ya Katiba, ametoa msamaha kwa wafungwa 5.704 kwa masharti,” amesema Simbachawene.
Hata hivyo, Simbachawene amesema Serikali inaweka utaratibu wa kufuatilia mienendo ya wafungwa watakaosamehewa na ikibainika wamerudia tena kujihusisha na makosa ya jinai, watarudishwa tena gerezani.
“Kumuachia mfungwa kama ameonesha tabia njema hatuwezi acha. Tutaweka utaratibu wa kuwafuatilia ambao wanajihusisha na makosa ya jinai, ili kabla hawajafanya makosa zaidi tuwarudishe gerezani,” amesema Simbachawene.
Simbachawene ametaja masharti ya kuachiwa huru wafungwa ikiwemo, wafungwa hao kupunguziwa robo ya adhabu zao baada ya punguzo la kawaida la moja ya tatu, inayotolewa chini ya kifungu cha 49 (1) cha Sheria ya Magereza Sura ya 58.
“Wafungwa hao sharti wawe wametumikia robo ya adhabu zao gerezani na wawe wameimgia gerezani kabla ya tarehe 9 Desemba 2021,” amesema Simbachawene.
Simbachawene amesema msamaha huo pia utawahusu wafungwa wenye magonjwa ya kudumu, wazee wenye umri wa miaka 70 au zaidi na wenye ulemavu wa mwili na akili na kuwa matatizo hayo yathibitishwe na Mganga Mkuu wa Mkoa au wa Wilaya.
“Sharti lingine, wafungwa wenye magonjwa ya ambayo hawana uwezo wa kumudu kufanya kazi, wafungwa wazee wenye umri wa miaka 70 au zaidi na wafungwa wenye ulemavu wa mwili na akili,” amesema Simbachawene.
Masharti mengine yaliyotajwa na Simbachawene, yanahusu wafungwa wa kike walioingia na mimba gerezani pamoja na wale walioingia na watoto wanaonyonya na wasionyonya.
Rais Samia Suluhu Hassan
“Wafungwa waliokaa gerezani kwa miaka 20 na kuendelea ambao wameonesha tabia njema, wafungwa waliohukumiwa adhabu ya kuwekwa kizuizini ambao wamekaa gerezani kuanzia miaka 15 na kuendelea,” amesema Simbachawene.
Aidha, Simbachawene amesema msamaha huo wa Rais Samia hautawahusu wafungwa wanaotumikia adhabu ya kunyongwa na wenye makosa ya kujaribu kuuwa, kujiuwa au kuuwa watoto wachanga.
Wengine ni, wafungwa wanaotumikia kifungo chini ya Sheria ya Bodi ya Patole, Sheria ya Huduma kwa Jamii na kifungo cha nje.
“Wengine ni wafungwa waliopatikana na hatia na kuhukumiwa kifungo kwa makosa ya sheria ya uhujumu uchumi ba wale wanaotumikia vifungo kwa makosa ya matumizi mabaya ya madaraka yao, utakatishaju fedha, rushwa na usafirishaji wa madawa ya kulevya,” amesema Simbachawene.
Simbachawene amewataja wengine kuwa ni “waliopatikana na hatia na kuhukumiwa kifungo kwa kosa la utekaji au wizi wa watoto, kufanya biashara ya binadamu, kuwapa mimba wanafunzi na ukatili dhidi ya watoto.”
Waziri huyo amesema, msamaha huo pia hauwahusu wafungwa waliokutwa na hatua na kuhukumiwa kifungo mwa kosa la kukutwa na viungo vya binadamu, wanaotumikia vifungo kwa makosa ya kujihusisha na nyara za Serikali na Ujangili.
Wanaotumikia vifungo kwa makosa ya wizi na ubadhirifu wa fedha za Serikali na wafungwa wanaotumikia vifungo kwa makosa ya kutoroka au kujaribu kitoroka chini ya ulinzi halali au kusaidia kutendeka kwa makosa hayo.
Leave a comment