SAMIA Suluhu Hassan, Rais wa Tanzania, amewaonya wabunge wanaojikita kumlinganisha yeye na aliyekuwa Rais John Pombe Magufuli, akiwataka kufanya kazi ya kibunge ikiwemo kujadili bajeti za wizara mbalimbali na si vinginevyo. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma … (endelea).
Rais Samia ametoa kauli hiyo leo Jumapili, tarehe 18 Aprili 2021, alipokuwa akihutubia kwenye kongamano la viongozi wa dini, lililofanyika ukumbi wa Chimwaga, mkoani Dodoma.
Kongamano hilo, lilikuwa na lengo la kuliombea taifa na viongozi wak na kumshukuru Mungu kwa maisha ya aliyekuwa Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli, aliyefariki dunia akiwa madarakani tarehe 17 Machi 2021.
Mara baada ya kifo hicho, Samia aliyekuwa makamu wa Rais, aliapishwa kuwa Rais wa Tanzania, tarehe 19 Machi 2021, kumalizika kipindi cha miaka minne ya utawala wa awamu ya tano, uliongia madarakani 5 Novemba 2020.
“Awamu ya sita, haikutokana na uchaguzi, haikutokana na chama kingine cha siasa, imetokana na Chama Cha Mapinduzi, awamu ni maneno tu, mambo ni yale yale.”
“Tutaendeleza mema yaliyokuwepo na kuleta mema mapya na ndiyo maana kauli mbiu yangu, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kazi Iendelee,” amesema Rais Samia
Huku akishangiliwa, Rais Samia amesema, ndiyo maana hata alipounda baraza la mawaziri, alifanya maboresho ya kuwahamisha baadhi “ni kuboresha tu na nitaendelea kuboresha.”
“Inasikitisha sana, watu wanapiga ngoma mitandaoni ila watu wanacheza bungeni.Mnalinganisha Magufuli na Samia, hawa watu ni kitu kimoja, nimekuwa nafuatilia mijadala bungeni, haina afya kwa taifa letu,” amesema Rais Samia.
Kauli hiyo, iliibua shangwe zaidi ukumbini na Rais Samia akasema “naomba sana, kipindi hiki wabunge, tunatakiwa kupitisha bajeti za sekta mbalimbali na mjikite sana huko na mengine tutayazungumza siku zinavyokwenda. Tufanye kazi kama Bunge linavyotakiwa kufanya kazi.”
Kauli hiyo ya Rais Samia, ameitoa kipindi ambacho kumeibuka mshuguano bungeni kwa wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), ambao wamegawanyika pande mbili.
Wanaotetea utawala uliopita wa Hayati Magufuli na wanaounga mkono kile kinachofanywa na Rais Samia.
Kuhusu suala la ugonjwa wa corona, Rais samia amesema, amekwisha kuunda kamati ya wataalamu ambao hivi karibuni atakutana nayo, lakini akatoa ombi kwa viongozi wa dini “niwaombe viongozi wa dini, waumini mnaowaongoza wachukue tahadhari zote kama kunawa mikono kwa maji tiririka, kutumia vitakasa mikono na kuvaa barakoa.”
Rais Samia amesema “ukiimngia kwenye mitandao ya kijamii, kuna uzandiki mkubwa wa watu kutunga maneno na niwaombe viongozi wa dini, mkemee yote yanayokwenda kinyume na maadili yetu ikiwemo kutobaguana kwa aina yoyote.”
“Napenda kuwahakikishia viongozi wa dini, kwa yale yote mliyoshauri, tumeyapokea na tutayafanyia kazi,” amesema Rais Samia
Leave a comment