RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewataka wasafirishaji wanaotumia pikipiki maarufu kama bodaboda nchini humo kuachana na vitendo vya wizi wa ukwapuaji na kushiriki vitendo vya ujambazi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dodoma…(endelea)
Mkuu huyo wa nchi ametoa wito huo leo Jumamosi tarehe 24 Julai, 2022, akizungumza nao kwa njia ya simu wakati wa kongamano la kuimarisha ushiriki wa madereva wa bodaboba na bajaji katika sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022.
“Ninyi ni maafisa usafirishaji wa Taifa lakini baadhi yenu wanawaharibia sifa yenu kwa kutumika kukwapua na kuiba mizigo ya watu lakini kutumika kwa ujambazi, niwaombe sana jilindeni msipoteze sifa yenu ninyi ni watu muhimu sana kwenye Taifa letu,” amesema Rais Samia.
Ameongeza kuwa bodaboda ni watu muhimu kwa kile alichoeleza kuwa ndiyo wasafirishaji wa wanyonge kwani gharama zao ni za chini.
“Tunapozungumzia usafiri wa wanyonge huo ndio usafiri wetu wanyonge ambao mnaweza kusafirisha watu kwa bei nafuu,” ameongeza.
Rais pia ameonesha kutambua uwepo wa wasomi katika kundi hilo na kuahidi kuzifanyia kazi changamoto zote watakazoeleza katika kongamano hilo.
Sekta yenu ni muhimu na najua kati yenu kuna wasomi wamo humo ndani, wenye diploma, wenye certificate (cheti), wenye shahada zao, niwaambie tu kwamba mama yenu nipo pamoja na ninyi, changamoto zote mtakazozungumza leo Mkuu wa Mkoa ataniletea ili tuzifanyie kazi,” amesema.
Leave a comment