RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, ametuma salamu za pole kwa Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi nchini, Jenerali Venance Mabeyo, kufuatia kifo cha Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Elias John Kwandikwa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Waziri Kwandikwa, amefikwa na mauti jana Jumatatu tarehe 02 Agosti, 2021 Jijini Dar es Salaam.
Rais Samia amesema amepokea kwa masikitiko taarifa za kifo cha Kwandikwa ambaye ni Mbunge wa Jimbo la Ushetu mkoani Shinyanga kutokana na mchango wake mkubwa katika utumishi wa umma.
“Tumempoteza mtu muhimu ambaye mchango wake katika utumishi wa umma hautasahaulika, Kwandikwa alikuwa kiongozi shupavu ambaye alikuwa akitekeleza majukumu yake kwa kuzingatia sheria na taratibu,” amesema Rais Samia.
Nasikitika kuwajulisha kuwa aliyekuwa Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Elias John Kwandikwa amefariki dunia. Nitakumbuka umahiri wake katika uongozi na uzalendo. Natoa pole kwa familia, Jeshi, Bunge na wananchi wa Jimbo la Ushetu. Mungu amweke mahali pema peponi, Amina pic.twitter.com/Wxte77dwuO
— Samia Suluhu (@SuluhuSamia) August 3, 2021
Rais Samia amemtaka Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi Jenerali Venance Mabeyo kufikisha salamu zake za pole kwa familia ya marehemh, ndugu, jamaa, marafiki na watu wote walioguswa na msiba huo.
Bwana ametoa na Bwana ametwaa jina lake lihimidiwe, Amina.
Salamu hizi za pole, zimetumwa kwa umma na Jaffar Haniu, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu.
Leave a comment