PANGA pangua ya Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, imewafyeka vigogo watano wa taasisi na idara za serikali. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Ni katika uteuzi alioufanya jana Jumapili tarehe 4 Aprili 2021, ikiwa ni mwendelezo wa kuunda safu yake ya uongozi huku wengine wakibadilishwia maeneo ya kazi.
Rais Samia aliingia madarakani tarehe 19 Machi 2021, akichukua nafasi ya Rais John Magufuli, aliyefariki dunia tarehe 17 Machi 2021, katika Hospitali ya Mzena, Makumbusho mkoani Dar es Salaam.
Soma zaidi:-
Tayari Rais Samia amefanya mabadiliko katika baraza lake la mawaziri, na sasa amegusa wakuu wa taasisi na idara za serikali.
Miongoni mwa vigogo waliofyekwa na panga la Rais Samia, ni pamoja na Dk. Edwin Mhede. Huyu alikuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ambapo nafasi yake imechukuliwa na Alphayo Kidata.
Dk. Mhende aliongoza mamlaka hiyo kwa mwaka mmoja na miezi tisa – kuanzia tarehe 8 Juni 2019, akichukua nafasi ya Charles Kichere, ambaye aliteuliwa kuwa Katibu Tawala, Mkoa wa Njombe.
Kabla ya uteuzi huo, Dk. Mhede alikuwa Naibu Katibu Mkuu Wizara ya Viwanda na Biashara.
James Kaji aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, ametupwa nje ambapo nafasi yake ikichukuliwa na Gerald Musabila.
Kaji alianza kwa kukaimu nafasi hiyo, baada ya aliyekuwa bosi wa mamlaka hiyo, Rogers Sianga kustaafu mwaka 2019.
Baada ya kukaimu nafasi hiyo, Hayati Magufuli alimthibitisha kuwa kamishna kuanzia tarehe 6 Julai 2020 na kumwapisha Ikulu ya Chamwino, Dodoma.
Kabla ya uteuzi huo mpya wa bosi wa mamlaka hiyo, Musabila alikuwa Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo.
Mwingine aliyewekwa kando ni James Kilaba, aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), nafasi yake ameteuliwa Dk. Jabir Bakari Kuwe.
Kabla ya uteuzi huo, Dk. Kuwe alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Serikali Mtandao.
Kwa upande wa Mfuko wa Hifadhi ya Jamii (NSSF), kibarua cha William Erio aliyekuwa mkurugenzi mkuu wa taasisi hiyo, kimeota nyasi baada ya Rais Samia kumteua Masha John Mshomba.
Erio alianza kuongoza taasisi hiyo tarehe 14 Julai 2018, akichukua nafasi ya Profesa Godius Kahyarara ambaye uteuzi wake ulitenguliwa na Hayati Magufuli.
Kabla ya uteuzi huo, Erio alikuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mfuko wa Pensheni (PPF).
Ikiwa ni takribani siku saba zimepita tangu Rais Samia kumsimamisha Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari (TPA), Deusdedit Kakoko, amemteua Erick Benedict Hamis kuongoza mamlaka hiyo.
Hadi anasimamishwa, Kakoko alikuwa ameongoza mamlaka hiyo kwa miaka minne na miezi tisa, kuanzia tarehe 25 Juni 2016 alipoteuliwa na aliyekuwa waziri wa ujenzi, uchukuzi na mawasiliano, Profesa Makame Mbarawa hadi tarehe 28 Machi 2021, Rais Samia alipomsimamisha.
Amesimamishwa ili kupisha uchunguzi wa tuhuma mbalimbali zinazoikabili mamlaka hiyo ikiwemo ubadhirifu wa fedha zaidi ya Sh.3 bilioni.
Mwingine aliyefekwa ni Emmanuel Ndomba, aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Meli Tanzania (TASAC), ambapo nafasi yake ametuliwa Kaimu Abdi Mkeyenge.
Ndomba aliteuliwa na Hayati Magufuli kuwa mkurugenzi mkuu tarehe 23 Aprili 2019.
Aliyeponea chupuchupu kuliwa kung’olewa ni James Mataragio, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), ambaye katika panga, panguo hiyo, alikuwa amewekwa kando na nafasi yake kuteuliwa Thobias Mwesiga Richard.
Hata hivyo, uteuzi wa Richard umedumu kwa saa zisizodizi 10 kabla ya Rais Samia, kutengua uteuzi wake na kumrejesha Mataragio kwenye nafasi hiyo.
Baadhi ya vigogo waliohamishwa vituo vya kazi ni Gerson Msigwa kutoka kuwa Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu na kuwa Mkurugenzi wa Idara ya Habari (Maelezo) na Msemaji Mkuu wa Serikali.
Pia, Profesa Abel Makubi ambaye alikuwa Mganga Mkuu wa Serikali, ameteuliwa kuwa Katibu Mkuu Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto.
Leave a comment