Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan amemtaka Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Pauline Gekul, kutetea wanawake katika michezo maana wanafanya vizuri lakini hawasifiwi. Anaripoti Kelvin Mwaipungu, Dar es Salaam … (endelea).
Maneno hayo amesema hii leo kwenye hafla ya kuwaapisha mawaziri na manaibu Waziri iliyofanyika Ikulu ya Chamwino jijini Dodoma.
Rais Samia alisema kuwa amempa mheshimiwa Gekul, wizara ya michezo ili akasaidie ikiwemo kutetea wanawake, kwani licha ya kufanya vizuri lakini hawasemwi kama ilivyo kwa timu za Taifa za wanaume ambao walipewa mpaka viwanja jijini Dodoma.
“Mheshimiwa Gekul nimempa Wizara ya michezo ili akasaidie pale, ikiwemo kutetea wanawake maana wanafanya vizuri lakini hawasifiwi,” amesema Rais Samia.
Aidha Rais Samia aliongezea kuwa timu za wanawake zilichukua makombe matatu lakini hawakusemwa tofauti na wanaume ambapo kelele zinakuwa nyingi hata kama hawajafika nusu fainali.
“Wamechukua makombe matatu hawasemwi ila wenzetu wanaume wakifunga goli, hata nusu fainali hawajafika utasikia kelele, mara wamepewa viwanja Dodoma,” alisema Rais Samia.
Gekul ameingia kwenye Wizara hiyo kuchukua nafasi ya Abdallah Ulega aliyepelekwa kuwa naibu waziri wa Ufugaji na uvuvi.
Mafanikio waliopata hivi karibuni wanawake kwenye michezo ni kutwaa Kombe Cosafa kwa timu ya taifa ya wanawake chini ya umri wa miaka 17.
Leave a comment