RAIS wa Tanzania, Dk. Samia Suluhu Hassan amewataka wafanyabiashara wa Zambia, kuitumia Bandari ya Dar es Salaam, kwa kuwa sasa inafanyiwa maboresho ili ifanye kazi zake kwa ufanisi. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam…(endelea).
Rais Samia ametoa wito huo leo tarehe 24 Oktoba 2023, akizungumza katika maadhimisho ya miaka 59 ya uhuru wa Zambia, yaliyofanyika jijini Lusaka, ambapo alipewa mwaliko wa kuwa mgeni rasmi na Rais wa taifa hilo, Hakainde Hichilema.
“Kwa sasa tunaboresha Bandari yetu ya Dar es Salaam, ili ifanye kazi kwa ufanisi na kwa wakati. Ningependa kuwaita jumuiya ya wafanyabiashara ambao nitaenda kukutana nao baada ya maadhimisho haya. Nawaita jumuiya ya wafanyabiashara kutumia nafasi hii ya kipekee,” amesema Rais Samia.
Katika hatua nyingine, Rais Samia ametoa hekta 20 zilizoko katika Bandari Kavu ya Kwala, kwa ajili ya wafanyabiashara wa Zambia kuzitumia, lengo likiwa ni kuwapunguzia gharama.
“Kutokana na mahusiano ya kibiashara kati ya nchi zetu, Serikali yangu imefanya maamuzi kutenga hekta 20 za ardhi ya Bandrai Kavu ya Kwala iliyoko mkoa wa Pwani, kwa ajili ya kuweka mizigo ya Zambia ili kupunguza gharama za kufanya biashara Zambia. Hii ndio zawadi ya Tanzania mnaposherehekea maadhimisho ya uhuru wenu,” amesema Rais Samia na kuongeza:
“Wakati mnasherehekea siku hii ya muhimu, nataka niwahakikishie kwamba Tanzania itaendelea kubaki kuwa mwanafamilia na mshirika wa Zambia, kama ilivyokuwa katika harakati za kupigania uhuru. Tutaendelea kuwa marafiki katika vipindi vyote, kuimarisha uchumi wetu na kuchukua hatua mbalimbali kuhakikisha tunaboresha njia zetu za usafirishaji,”amesema.
Kwa upande wake Rais Hichilema, amemtaka Rais Samia washirikiane katika kuendeleza mikakati iliyoasisiwa na waasisi wa mataifa hayo, Mwalimu Julius Nyerere (Tanzania) na Keneth Kaunda (Zambia), kwa ajili ya kuimarisha mahusiano na maendeleo ya pande zote mbili.
“Pindi njia yetu ya Kusini imefungwa wakati wa harakati za kupigania uhuru,viongozi wetu wa kweli, Mwalimu Nyerere na Kaunda walifanya kazi pamoja kufungua hiyo njia kupitia arhdi ya Tanzania na Zambia kupitia reli ya TAZARA na kuanzisha bomba la mafuta na mikakati mingine ambayo sisi inatunufaisha sasa. Hivyo tuna kazi ya kuimarisha na kuendeleza yale waliyoanzisha,” amesema Rais Hichilema.
Rais Hichilema amezungumzia umuhimu wa kuboresha miundombinu ya usafirishaji kati ya Zambia na Tanzania, ikiwemo reli na bomba la mafuta.
Kiongozi huyo wa Zambia, amesema nchi yake na Tanzania wana jukumu kubwa la kuboresha reli ya TAZARA na kupanua bomba la mafuta.

Pia, amehimiza ushirikiano baina ya nchi zote mbili katika sekta za gesi, nishati safi, barabara, mawasiliano, teknolojia ya kidigitali, chakula, biashara na ajira, kwa kutumia rasilimali zake.
“Hili ni jukumu letu lisiloepukika, kuendeleza mambo haya kwa kutumia rasilimali tulizozawadiwa na Mungu ili kuboresha maisha ya wananchi wetu,” amesema Rais Hichilema.
Akizungumzia kuhusu miaka 59 ya uhuru wa Zambia, Rais Hichilema amesema serikali yake itaendelea kutumia rasilimali zake katika kuhakikisha zinaimarisha uchumi na maisha ya wananchi wake.
“Kwa sasa serikali yangu inaendelea kubeba jukumu la kuboresha uchumi na uhuru wa kijamii, kwa kuongeza viwango vya mishahara, kugawa rasilimali zilizopo kwa ajili ya uwekezaji na biashara ili kukuza uchumi ambapo tutaweza kutengeneza ajira kwa watu wetu, kutoa elimu bure ambapo tangu tumeanza kutekeleza sera ya elimu bure madarasa yamejaa wanafunzi waliokuwa nje ya shule,” amesema Rais Hichilema na kuongeza:
“Kwa hiyo tutawahudumia wagonjwa, watu wenye ulemavu, wazee na wastaafu. Tunaweza tukafanya hivi vyote lwa kutumia rasilimali ambazo Mungu ametupatia.”
Leave a comment