RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amefanya uteuzi wa viongozi sita wa taasisi mbalimbali. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Uteuzi huo umetangazwa leo Jumatano, tarehe 21 Aprili 2021 na Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais, Ikulu ya Tanzania.
Msigwa amewataja walioteuliwa ni;
1. Dk. Jones A. Kilimbe kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
Dk. Kilimbe anaendelea na wadhifa huo kwa kipindi cha pili baada ya kipindi cha kwanza kumalizika.
2. Amemteua Hab Mkwizu kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Magazeti ya Serikali (TSN).
Mkwizu anaendelea na wadhifa huo kwa kipindi cha pili baada ya kipindi cha kwanza kumalizika.
3. Amemteua Yahaya Ibrahim Mgawe kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Taasisi ya Utafiti na Uvuvi Tanzania (TAFIRI).
4. Amemteua Prof. Erick Vitus Komba kuwa Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi ya Utafiti wa Mifugo Tanzania (TALIRI).
Prof. Komba amechukua nafasi ya Dk. Eligy Mussa Shirima ambaye amestaafu.
5. Amemteua Kadari Singo kuwa Afisa Mtendaji Mkuu wa Taasisi ya Uongozi. Singo amechukua nafasi ya Prof. Joseph Semboja ambaye amestaafu.
Msigwa amesema, uteuzi wa viongozi hao umeanza jana Jumanne, tarehe 20 Aprili, 2021.
Msigwa amesema, Rais Samia, amemteua Dk. Natu El-Maamry Mwamba kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Kampuni ya Uendeshaji wa Kiwanja cha Ndege cha Kilimanjaro (KADCO). Uteuzi wa Dk. Mwamba umeanza tarehe 19 Aprili, 2021.
Leave a comment