RAIS Samia Suluhu Hassan, amesema Serikali yake itaendelea kutoa fedha kwa ajili ya utekelezaji wa mipango ya sekta ya maji, ili kuongeza upatikanaji wa huduma hiyo muhimu kwa wananchi. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ametoa ahadi hiyo leo Ijumaa, tarehe 11 Novemba 2022, akizindua mradi wa maji Kigamboni, jijini Dar es Salaam.
Mkuu huyo wa nchi, amemuagiza Waziri wa Maji, Jumaa Aweso, atumie mitambo ya maji iliyonunuliwa na Serikali, kuufufua Wakala wa Uchimbaji Visima na Ujenzi wa Mabwawa.
“Niseme mitambo hii ni mali kubwa sana kwa taifa letu na kama itatumika ipasavyo itakwenda kufanya kazi kubwa sana. Kuna suala la waziri kuomba taasisi ya wakala wa uchimbaji visima iende kufufuliwa, sasa waziri hili ni lako nenda kajipange uwezavyo ninachotaka mimi kuona mitambo inaenda kufanya kazi inayoonekana Tanzania yote,” amesema Rais Samia.
Katika hatua nyingine, Rais Samia ameagiza Wizara ya Maji kutumia ipasavyo vifaa vya utafiti wa maji, ili kuokoa fedha za Serikali kwa kuchimba maeneo sahihi yenye maji.
“Huko nyuma tulikuwa na miradi kadhaa na mradi unaojulikana kwa wepesi zaidi ni mradi wa visima 10 kila mkoa, fedha nyingi ya Serikali ilitumika na hakuna visima vilivyotoa maji, nadhani ni asilimia 10 ya ule mradi ndio ulikuja na matokeo chanya lakini sehemu iliyobakia yote fedha ilipotea maji hayakupatikana,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema “Sasa hivi vifaa vitatuambia kwa hakika maji yako hapa chimba, sasa mtu aje kuchimba kisima huku vifaa anavyo na kisima hakitoi maji, aidha Aweso au yeye. Kabla ya huyo mtu kufikishwa kwangu Aweso ajitambue, kama wakilishughulikia nawahakikishia nafasi zao.”
Aidha, Rais Samia amesema, Serikali yake itafanyia kazi mapendekezo yaliyotolewa na kamati iliyoundwa 1990 kuangalia namna ya kuvuna maji ya mvua, ili kukabiliana na changamoto ya upungufu wa maji wakati wa ukame.
“Katika miaka ya 1990 Tanzania hii iliunda kamati ya kuangalia jinsi tutakavyoweza kuvuna maji ya mvua na katika kamati ile nilikuwa mjumbe kutoka Zanzibar,tulifanya kazi kubwa lakini haikutekelezwa. Tuliotoa mapendekezo mengi lakini hayakutekelezwa, leo hii Mungu ametuweka hai tunakwenda kuyatekeleza yale tuliyopendekeza,” amesema Rais Samia.
Leave a comment