RAIS Samia Suluhu Hassan, amemuagiza Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), Jaji Eliezer Feleshi kufanya mchakato wa marekebisho ya Sheria ya Ubia kati ya Sekta ya Umma na Sekta Binafsi (PPP), pamoja na ya Manunuzi ya Umma, ili kuondoa vifungu vinavyokwamisha masuala ya uwekezaji na biashara. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Rais Samia ametoa maagizo hayo leo Jumatatu, tarehe 4 Julai 2022, akizungumza katika hafla ya utiaji saini mktaba wa ujenzi wa Reli ya Kisasa, jijini Dar es Salaam.
“Mwanasheria mkuu uko hapa, sheria yetu ya PPP na sheria ya manunuzi, hizo sheria zikafaniwe kazi. Sheria kazitazameni ili badili ya kutupeleka mbele inaturudisha nyuma,”amesema Rais Samia.
Amesema, jukumu la Serikali ni kuweka mazingira mazuri kwa sekta binafsi katika kufanya biashara na kunufaika na fursa zinazopatikana nchini, hasa kwa mashirika ya ndani.
“Dunia ya sasa anakuja mtu ana uwezo mnamuamini, mnasaini mikataba mnakwenda mbele. Kuanza kuzunguka sheria ya PPP haijafuatwa, single source haijafuatwa, miezi mitatu minne mtu ana pesa zake anatafuta pa kwenda, ukiuliza kimya oooh sheria hairuhusu imekwama hapa,” amesema Rais Samia.
Rais Samia amesema “sheria tumetunga wenyewe, kwa nini tunakuwa watumwa wa sheria tunazotunga. Naomba mkatazame hizo sheria za PPP na manunuzi.”
Katika hatua nyingine, Rais Samia amewajibu watu wanaobeza ziara zake za nje ya nchi, akisema anazifanya kwa kuwa kuna fursa za maendeleo.
“Wenye akili za kawaida ni rahisi kulaumu, Rais anasafiri tu hakai. Badala ya kutembelea mikoa anatembelea tu nje, lakini matokeo yake ndiyo haya. Nikienda mkoani tunajenga siasa ya ndani, hakuna maendeleo. Nikienda nje nakwenda kutafuta fedha kwa ajili ya maendele,” amesema Rais Samia.
Leave a comment