RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, amewaagiza wakuu wa mikoa na wilaya, kufufua mabaraza ya biashara katika maeneo yao. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es salaam…(endelea).
Ametoa gizo hilo leo Jumamosi, tarehe 26 Juni 2021 alipozungumza katika mkutano wa 12 wa Baraza la Taifa la Biashara (TNBS), Jijini Dar es Salaam.
Kiongozi huyo amewaagiza wateule wake kushirikiana na sekretarieti ya TBNS, katika kufufua mabaraza hayo.
“Nawaagiza wakuu wa mikoa na wilaya zote, ambao ni wenyeviti wa mabaraza katika maeneo yao. Kushirikiana na sekretarieti ya Baraza la Taifa, ili kuhakikisha mabaraza hayo yanafanya kazi,” amesema Rais Samia.
Ameeleza ufufuaji wa mabaraza hayo, utakuwa chachu kwa maendeleo ya TBNS.
“NisisItize umuhimu wa mabaraza ya mikoa na wilaya kuyapa uhai na kufanya kazi. ufanisi wa baraza la taifa utategemea utendaji kazi wa mabaraza ya mikoa na wilaya,”
“Sababu tunapozungumzia biashara na uwekezaji sio Dar es Salaam na Dodoma peke yake au miji mikuu peke yake, lakini ni mpaka chini kwenye mikoa na wilaya,” amesema Rais Samia.
Akizungumzia utendaji wa TBNS, Rais Samia amesema baraza hilo tangu lianzishwe 2001, limesaidia uboreshaji wa sera, sheria, kanuni na taratibu za biashara nchini.
“Baraza limekuwa chachu katika kujadili, kuboresha na kuaunzisha sera, kanuni, taratibu za biashara na uwekezaji,” amesema Rais Samia.
Amesema Serikali yake itaendelea kulilea baraza hilo, ili kuendeleza azma ya uundwaji wake.
“2001 Serikali yetu iliamua kuanzisha baraza hili la taifa la baishara, ina maana kuwa mwaka huu limetimiza miaka 20 toka kuanzishwa kwake,” amesema Rais Samia na kuongeza:
Lengo kuu litumike kama chombo ama jukwaa rasmi la majadiliano kati ya Serikali na sekta binafsi, ili kuwezesha kupatikana muafaka ama uelewa wa pamoja kuhusu masuala muhimu yanayohusu maboresho ya biashara na uwekezaji nchini.”
Leave a comment