RAIS wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan ameliagiza Jeshi la Polisi nchini humo kurekebisha sheria ya kuweka mtu mahabusu pamoja na kufuta kesi ambazo upelelezi wake hautokamilika. Anaripoti Gabriel Mushi, Dar es Salaam … (endelea).
Rais Samia ametoa agizo hilo leo Jumatano, tarehe 25 Agosti, 2021 wakati akifungua kikao kazi cha maofisa wakuu waandamizi wa jeshi la polisi na makamanda wa polisi wa mikoa/vikosi – Oysterbay Dar es Salaam.
Amesema kwa kuwa jeshi la polisi limejiwekea utaratibu kwamba ukomo wa upelelezi wa kesi ndogo kuwa miezi sita wakati kesi kubwa kuwa mwaka mmoja, sasa kwa kuwa kesi ambazo upepelezi hautokamilika mahabusu hao watolewe.
“Kwa zile kesi ambazo upelelezi hautakamilika watolewe wakafaidi uhuru wao hili nalisema kwa mara ya pili au ya tatu,” amesema Rais Samia akimtaka Inspekta Jenerali wa Polisi (IGP), Simon Sirro kulifanyia kazi hilo
Rais Samia amesema hadi kufikia tarehe 22 Agosti 2021, idadi ya mahabusu katika jela zote nchini ni karibu sawa na wafungwa wote.
“Hadi juzi wafungwa walikuwa 16,542 wakati mahabusu 15,194,” amesema.
“Nataka mrekebishe sheria ya kuweka mtu mahabusu kwa sababu nchi nyingine mtu hakamatwi hadi upelelezi ukamalike, serikali inabeba mzigo wa maelfu ya mahabusu wakati upelelezi haujakamilika, naomba muangalie hayo ili mtoe huduma zinazofaa kwa watu wetu,” amesema Rais Samia.
Leave a comment