RAIS mpya wa Kenya, William Ruto, ametangaza baraza lake la mawaziri, lenye mawaziri 21. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Kiongozi huyo wa tano wa Kenya, ametangaza baraza hilo leo Jumanne, tarehe 27 Septemba 2022, ikiwa ni siku kadhaa tangu aapishwe kuwa Rais wa taifa hilo, akichukua mikoba ya mtangulizi wake, Uhuru Kenyatta aliyemaliza muda wake.
“Huu ndiyo uteuzi nilioufanya mchana huu, uteuzi mwingine utafuata katika maeneo mengine ambayo ni sehemu ya timu ambayo itafanya kazi na mimi na kaka zangu wawili na baraza zima kuhakikisha tunatekeleza mipango na program ambazo wananchi wa Kenya wametuchagua kufanya,” amesema Rais Ruto.
Akitangaza baraza hilo kupitia matangazo ya moja kwa moja, yaliyorushwa na vyombo vya habari nchini Kenya, Rais Ruto amesema amemteua Profesa Kithure Kindiki, kuwa Waziri wa Mambo ya Ndani na Utawala wa Kitaifa, huku Profesa Njuguna Ndung’u, akimteua kuwa Waziri wa Hazina ya Taifa na Mipango.
Rais Ruto amemteua Aisha Jumwa, kuwa Waziri wa Utumishi wa Umma, Jinsia na Hatua Madhubuti; Aden Duale amemteua kuwa Waziri wa Ulinzi; Alice Wahome, ameteuliwa kuwa Waziri wa Maji, huku Alfred Mutua, akimteua kuwa Waziri wa Mambo ya Nje na Masuala ya Diaspora.
Moses Kuria, ameteuliwa na Rais Ruto kuwa Waziri wa Biashara, Uwekezaji na Viwanda; Rebecca Miano, ameteuliwa kuwa Waziri wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC), Ardhi Kame na Maendeleo ya Kikanda. Katika Wizara ya Barabara, Raius Ruto amemteua Kipchumba Murkomen, kuwa waziri wake.
Pia, Rais Ruto amemteua Roselinda Soipan, kuwa Waziri wa Mazingira na Zacharia Mwangi, kuwa Waziri wa Ardhi, wakati Peninnah Malonza, akimteua kuwa Waziri wa Utalii, huku Mithika Linturi, akimteua kuwa Waziri wa Kilimo.
Katika Wizara yaAfya, Rais Ruto amemteua Susan Nakhumicha, kuiongoza; Eliud Owalo, ameteuliwa kuwa Waziri wa Habari, Mawasiliano na Uchumi wa Kidigitali; Ezekiel Machogu, amemteua kuwa Waziri wa Elimu na Davis Chirchir, amememteua kuwa Waziri wa Nishati na Mafuta.
Rais Ruto amemteua Ababu Namwamba, kuwa Waziri wa Michezo; Simon Chelugui, kuwa Waziri wa Ushirikiano na Viwanda Vidogo na vya kati; Salim Mvurya, ameteuliwa kuwa Waziri wa Madini, Uchumi wa Buluu na Masuala ya Baharini na Florence Bore, ameteuliwa kuwa Waziri wa Kazi.
Leave a comment