RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi, ametoa salamu za rambirambi kwa Mama Janeth Magufuli, familia pamoja na Makamu wa Rais wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan na wananchi wote wa Tanzania kufuatia kifo cha Rais wa taifa hilo, Dk. John Pombe Magufuli. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea)
Katika salamu hizo za rambirambi, Rais Mwinyi, amesema, amepokea kwa masikitiko makubwa taarifa ya kifo cha Rais wa Tanzania, John Pombe Magufuli kilichotokea jana Jumatano tarehe 17 Machi 2021, mkoani Dar-es-Salaam alipokuwa akipatiwa matibabu.
Salamu hizo za Rais Mwinyi, zimeeleza, huu ni msiba mzito sana kwake na kwa taifa la Tanzania, hivyo aliwaomba wananchi kuwa na subira na utulivu katika kipindi hichi kigumu cha msiba huu mzito wa kitaifa.
Kwa niaba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar na wananchi wote wa Zanzibar, Rais Mwinyi alitoa salamu hizo za rambirambi na kumuomba Mwenyezi Mungu ailaze roho ya Marehemu mahala pema peponi, Amin.
Leave a comment