RAIS wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi anaamini watu wanaohoji na kupinga miradi inayoanza kutekelezwa hapa Zanzibar ni wapinzani wake. Anaripoti Jabir Idrissa, Zanzibar … (endelea).
Akizungumza na Wahariri na Waandishi wa Habari kwenye mkutano wake wa kila mwezi na vyombo vya habari jana Jumatatu tarehe 28 Februari 2022, Rais Mwinyi alisema wananchi wenye nia nzuri na uongozi wake wanajua kinachoendelea.
Rais Mwinyi alisema shida ni wale wasiokuwa na nia njema naye ambao alisema wamezoea kupinga tu kila kinachofanywa.
“Nimekuelewa. Lakini sidhani kama watu hawajui tunachokifanya. Labda wanaotoka vijijini hawajui lakini mjini watu wanajua kuwa tunatekeleza miradi mbalimbali. Kuna watu wao ni upinzani tu…hawa hawafurahii tunavotekeleza ilani. Wengine wanajua,” alisema.
Alisema haitachukua muda mrefu wanaohoji wataelewa nia nzuri ya uongozi wake wa awamu ya nane kwa kuona maendeleo kwenye maeneo yalikozungushiwa uzio wa mabati.
Rais Mwinyi alisema hayo kwa njia ya kutoa ufafanuzi baada ya kupewa nasaha kuwa asiudhike na maneno yanayosemwa na wananchi kuhusu hatua ya maeneo mengi hususan ndani ya jiji la Zanzibar kuzungushiwa uzio wa mabati.
Mwandishi wa habari hizi aliyehudhuria mkutano huo uliofanyika ukumbi wa Ikulu ya Zanzibar alimuomba Rais kutoudhika badala yake azingatie dhana ya utawala bora inayohimiza uwazi kwa kueleza malengo ya serikali kwenye maeneo hayo kupitia mabango yanayoeleza aina ya mradi, mfadhili wake, mjenzi wake, msanifu wa ujenzi na kadhalika.
Ni baada ya kumsikia Rais mwenyewe akigusia suala hilo hivi karibuni akiwa kwenye ibada ya sala ya Ijumaa; na hapo jana wakati akitoa maelezo ya utangulizi kabla ya kukaribisha maswali ya waandishi wa habari wakiwemo wajumbe wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) waliotoka Dar es Salaam.
Kumekuwa na maneno yakisemwa na wananchi kwenye baraza mbalimbali wakishangaa na kuhoji wanachokiona “kuzidi” kwa uzio wa mabati kwenye maeneo mbalimbali jijini.
Baadhi ya maeneo hayo ni yanayoonekana kuwa ni ya wazi ambayo hayakutarajiwa kujengwa majengo kwa ajili ya makazi au biashara.
Rais akiwa Msikiti wa Kijitoupele Ijumaa iliyopita, alisema wananchi na hasa wanaohoji wataelewa pale ujenzi utakapokamilika na mabati kuondolewa.
Katika hatua nyengine, Rais Mwinyi amesema serikali inatambua jukumu muhimu la kujiandaa na kuajiri madaktari wengi zaidi kwa ajili ya kutosheleza mahitaji mapya ya wataalamu hao baada ya kukamilika kwa ujenzi wa hospitali ngazi ya wilaya kote Unguja na Pemba pamoja na urekebishaji wa Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja ambayo ndio ya rufaa.
Ujenzi huo unatekelezwa kwa fedha zilizotolewa kwa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ajili ya kupunguza makali ya ugonjwa wa Covid-19. Fedha hizo zimetolewa na Shirika la Fedha la Kimataifa (IMF).
Leave a comment