RAIS wa Zanzibar, Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema, atawachukulia hatua kali watumishi watakaoshindwa kutekeleza majukumu yao kwa kigezo cha kusubiri maagizo kutoka kwa viongozi wa juu. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Rais huyo wa awamu ya nane wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ametoa onyo hilo leo Jumanne tarehe 11 Novemba 2020, wakati anazindua Baraza la 10 la Wawakilishi Zanzibar sambamba na kutoa dira ya Serikali atakayoiongoza.
Amewatahadharisha viongozi na watumishi wa umma atakaowateua, hatowavumilia watumishi watakaosubiri maelekezo nini wafanye katika utekelezaji wa majukumu yao.
“Napenda viongozi wote nitakaowateua wazingatie hili. Serikali haitavumilia viongozi watakaosubiri kuambiwa nini wafanye katika kutekeleza majukumu yao,” amesema Rais Mwinyi.
Aidha, Rais Mwinyi amesema “Serikali haitakuwa na muhali kwa mtendaji ambaye hatawajibika katika utekelezaji wa majukumu yake, atakayeshindwa kuwajibika aelewe atawajibishwa.”

Akielezsa dira ya Serikali yake, Rais Mwinyi amesema, itajikita katika kuimarisha uchumi wa Zanzibar kwa kutumia bahari, kupitia sekta ya uvuvi, usafirishaji na utalii.
Amesema, Serikali yake itaboresha huduma za kijamii ikiwemo afya, miundombinu, maji na elimu.
Pia, amesema katika teuzi atakazozifanya zitazingatia taalamu na uwajibikaji ili kuwa na watendaji watakaowatumikia wananchi ipasavyo.
Kuhusu sekta ya afya, Rais Mwinyi ameahidi kutoa huduma za afya bure kwa wananchi wasiokuwa na uwezo huku akiahidi kuanzisha bima ya afya kwa wananchi wenye uwezo.
“Tutaangalia uwezekano wa kuanzisha bima ya afya kwa wenye uwezo na wasiokuwa na uwezo serikali itaendelea kuwapatia huduma ya afya bure,” amesema Rais Mwinyi.

Ameahidi, kuwatunza wazee kwa kuhakikisha wanapata matibabu bora, chakula na malazi.
“Serikali itaendelea kuwatunza wazee. Wazee wanaoishi katika kambi tutawapatia huduma za muhimu chakula na matibabu zitaendelea,” ameahidi Rais Mwinyi..
Ameahidi kulinda haki za wanawake, watoto na wazee kwa kukomesha vitendo vya unyanyasaji.
Rais Mwinyi amesema, ili kukabiliana na changamoto ya ukosefu wa ajira, Serikali yake itaanzisha sera nzuri zitakazotoa kipaumbele kwa Wazanzibar kupata ajira.
“Serikali itandaa sera nzuri za ajira zitakazolazimisha wawekezaji kutoa kipaumbele katika utoaji kazi kwa Wazanzibar,” amesema Rais Mwinyi.
Aidha, Rais Mwinyi amesema, mageuzi makubwa ya uchumi yatazalisha ajira nyingi kwa vijana, huku akiahidi kutoa mikopo kwa vijana ili wajiajiri na kuondokana na hali ya utegemezi.
“Mapinduzi makubwa ya uchumi yatapelekea ukuaji uchumi wa kisasa na kuongeza fursa za ajira, ni wajibu wa vijana kuwa tayari kufanya kazi. Vijana watawezeshwa kupata mitaji ili wajiajiri wenyewe na kuondokana na tatizo la kutegemea ajira chache serikalini,” amesema Rais Mwinyi.
Mara baada ya kulizindua baraza hilo, liliahirishwa hadi tarehe 10 Februari 2021 litakapokutana tena saa 3:00 asubuhi.
Leave a comment