RAIS wa Zanzibar, Hussein Ali Mwinyi, amefanya uteuzi wa wanachama wawili wa ACT-Wazalendo kuwa Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar … (endelea).
Walioteuliwa ni; Mwanasheria Mkuu wa ACT-Wazalendo, Omar Said Shaaban na Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho-Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui.
Taarifa ya Katibu Mkuu Kiongozi Zanzibar, Dk. Abdulhamid Mzee imesema, uteuzi wa wawili hao unaanza leo Jumatatu tarehe 07 Desemba 2020.
Uteuzi huo ni mwendelezo wa Rais Mwinyi kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa ikihusisha vyama vya CCM na ACT-Wazalendo kwa mujibu wa Katiba.
Jana Jumapili, Rais Mwinyi alimteua Mshauri Mkuu wa ACT-Wazalendo, Maalim Seif Sharif Hamad kuwa Makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar.
Uteuzi huo aliufanya saa chche kupita tangu Katibu Mkuu wa ACT-Wazalendo, Ado Shaibu kuwaeleza wanahanari jijini Dar es Salaam kwamba, kikao cha kamati kuu ya chama hicho, kimeridhia kwenda kuunda Serikali ya Umoja wa Kitaifa.
Katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika tarehe 27 na 28 Oktoba 2020, Chama Cha Mapinduzi (CCM) kilishinda nafasi ya urais kwa asilimia 76 na ACT-Wazalendo kikishika nafasi ya pili kwa asilimia 19.
Leave a comment