RAIS wa Zanzibar, Dk. Hussein Mwinyi ametengua uteuzi wa Kamishna wa Bodi ya Mapato Zanzibar (ZRB), Joseph Meza na Mkurugenzi Mwendeshaji wa Benki ya Watu wa Zanzibar (PBZ), Iddi Haji Makame. Anaripoti Mwandishi Wetu, Zanzibar…(endelea).
Taarifa hiyo imetolewa leo Alhamisi tarehe 11 Februari 2021 na Katibu wa Baraza la Mapinduzi ambaye pia ni Katibu Mkuu Kiongozi, Zanzibar, Zena Said.
Kwa mujibu wa taarifa ya Zena, viongozi hao ambao teuzi zao zimetenguliwa, watapangiwa kazi nyingine.
“Kamishna wa Bodi ya Mapato na Mkurugenzi Mwendeshaji wa PBZ, waliotenguliwa watapangiwa kazi nyingine kadri itakavyoamuliwa,” inaeleza taarifa ya Zena.
Wakati huo huo, taarifa hiyo inasema, Rais Mwinyi amemteua Salum Yussuf Ali kuwa Kamishna wa ZRB na Dk. Muhsin Salim Masoud, amemteua kuwa Mkurugenzi Mwendeshaji wa PBZ.
“Rais Mwinyi amewateua wafuatao kushika nyadhifa ZRB na PBZ katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kama ifuatavyo, Ali ameteuliwa kuwa Kamishna wa ZRB na Dk. Masoud ameteuliwa kuwa Mkurugenzi Mwendeshaji PBZ,” inaeleza taarifa hiyo.
Taarifa ya Katibu Mkuu huyo Kiongozi wa Zanzibar, imeeleza uteuzi wa viongozi huo umeanza jana Jumatano tarehe 10 Februari 2021.
Hatua hiyo ya Rais Mwinyi kufanya mabadiliko ya uongozi katika ZRB na PBZ imekuja siku mbili baada ya kueleza miakati yake ya kuimarisha ukusanyaji wa mapato visiwani humo.
Tarehe 9 Februari 2021, wakati akizungumza na wanahabari kuhusu siku 100 za uongozi wake tangu alipoapishwa tarehe 2 Novemba 2020, kuiongoza Serikali ya awamu ya nane Zanzibar, Rais Mwinyi alisema atadhibiti mianya yote ya upotevu wa mapato.
Kwa nini wasichukuliwe hatua za kisheria kwa kufikishwa mahakamani? Badala yake wanaachiliwa wakale kwengineko