RAIS wa Uganda, Yoweri Museveni amesema aliona mapema anguko la vyama vya upinzani kwenye Uchaguzi Mkuu uliofanyika Jumatano tarehe 28 Oktoba 2020. Anaripoti Mwandishi Wetu…(endelea).
Rais Museveni amesema hayo leo Alhamisi tarehe 5 Novemba 2020 katika sherehe za kuapishwa Dk. John Pombe Magufuli kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania iliyofanyika Uwanja wa Jamhuri jijini Dodoma.
Dk. Magufuli wa chama tawala-CCM alitangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuwa mshindi wa uchaguzi huo akipata kura milioni 12 kati ya milioni 15 zilizopigwa sawa na asilimia 84 huku Tundu Lissu wa Chadema akipata kura milioni 1.9 sawa na asilimia 13.
Katika uchaguzi huo, umeshuhudia vyama vya upinzani vikipoteza madiwani na wabunge wengi akiwemo aliyekuwa kiongozi wa kambi rasmi ya upinzani bungeni, Freeman Mbowe.

Mbowe ambaye ni Mwenyekiti wa Chadema, alishindwa kutetea Jimbo la Hai Mkoa wa Kilimanjaro ambalo lilikuwa la kwanza kutangazwa matokeo kwa Shaashisha Mafuwe wa CCM aliibuka mshindi.
Akitoa salamu zake kwenye sherehe hizo, Rais Mseven amesema, anguko hilo aliliona alipofuatilia matokeo ya awali ya uchaguzi huo kupitia Televisheni ya Taifa (TBC) na kuona upinzani unapoteza Jimbo la Hai na majimbo mengine tofauti ilivyokuwa katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.
“Safari hii, niliweka tena TBC One nikaona Hai, hayo ndio majimbo walitangaza kwanza Hai na majimbo mengine Newala huko Mtwara nikasema basi,” amesema Rais Museveni huku akiibua shangwe uwanjani hapo na watu wakiimba CCM, CCM, CCM…
Wakati huo huo, Rais Museveni amesema katika Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015 alikuwa na hofu juu ya ushindi wa CCM lakini alipata nguvu baada ya kuona chama hicho kimeshinda kwa kura nyingi katika Jimbo la Ilemela ambapo alishinda Angelina Mabula wa CCM.
“Huwa natazama TBC kujua siasa zenu, uchaguzi wa 2015 nilikua na hofu sana imekuaje hii, lakini baadae nikaona mama mmoja alichaguliwa kwa kura nyingi sana, alitoka jimbo la Ilemela nikasema inaonekana watu wetu wako huko,” amesema Museveni.
Rais Museveni amesema, alijua kama CCM kingeshinda kwa kuwa anajua muelekeo wa kisiasa wa chama hicho tofauti na vyama vingine.
“Kawaida nafuatilia mambo ya Tanzania lakini wakati wa uchaguzi nakuja naweka TV yenu TBC naanza kutazama na kuona huu uchaguzi unakuja vipi na hii sababu naujua mueleleo wa CCM kisiasa hivi vyama vingine sijui mwelekeo,” amesema Rais Museveni.
Natumia wakati huu kupongeza umma wa watanzania kumchagua MTU anayefanana na maendeleo lakini pia kwa kuapishwa rais magufuli-hongera sana!naomba ufanye kazi kwa juhudi kama watanzania tulivyokuamini na mungu wetu atakusaidia !utanzania kwanza mengine baadaye