BENJAMIN William Mkapa, Rais mstaafu wa awamu ya tatu ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amehitimisha safari yake ya miaka 81 dunia. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam … (endelea).
Mkapa aliyeiongoza Tanzania kwa miaka kumi kati ya mwaka 1995-2005, amefariki dunia usiku wa kuamkia leo Ijumaa tarehe 24 Julai 2020 katika moja ya Hospitali jijini Dar es Salaam nchini Tanzania.
Taarifa za kifo chake, zimetolewa na Rais wa nchi hiyo, John Pombe Magufuli saa 6 usiku wa kuamkia leo na tayari ametangaza siku saba za maombolezo ambapo bendera zote zitapepea nusu mlingoti.
Soma zaidi:-
Mkapa amefariki ikiwa ni takribani miezi tisa tangu kilipozinduliwa Kitabu chake cha “My Life, My Purpose” (Maisha Yangu, Kusudi Langu). Katika kitabu hicho, anajutia na kukubali kubeba lawama zote kwa baadhi ya matukio, huku akieleza somo alilopata.
Kitabu hicho kilizinduliwa na Rais Magufuli tarehe 12 Novemba 2019 siku aliyoadhimisha miaka 80 ya kuzaliwa kwake, katika ukumbi wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.
https://youtu.be/cEIgBhzKseQ
Miongoni mwa yale ambayo Mkapa aliyezaliwa tarehe 12 Novemba mwaka 1938, amezungumzia umuhimu wa uwepo wa Tume Huru ya Uchaguzi ambapo hadi anafikwa na mauti, hitajio hilo na ndoyo ya kuona uwepo wa Tume huru halijatimia.
Katika kitabu hicho, Mkapa anasema kuundwa kwa tume huru ya uchaguzi ni njia mojawapo ya kuondoa manung’uniko ya vyama vya siasa na kuimarisha demokrasia barani Afrika huku akijutia mauaji yaliyotokea Zanzibar Januari 26 na 27 mwaka 2001 akisema yalitia doa utawala wake.
Mkapa anasema ili kuwa na usawa katika mfumo wa vyama vingi nchini, ni muhimu kuwa na chombo huru kilichojumuisha vyama vyote.
“Kuundwa kwa tume huru ya uchaguzi itakayokubalika na vyama vyote vya siasa ndio chachu ya kulea na kukuza demokrasia nchini,” anasema Mkapa, ambaye anasema alipata funzo kubwa la umuhimu wa kushirikiana na vyama vya siasa baada ya mauaji ya wafuasi 22 wa CUF yaliyofanywa na polisi kisiwani Pemba Januari 26 na 27 mwaka 2001.
Mkapa anatahadharisha muundo wa tume umekuwa miongoni mwa masuala yanayopigiwa kelele na kupata upinzani mkubwa kutokana na upatikanaji wa viongozi wake.
Anashauri mamlaka ya nchi inaweza kubaki na mamlaka ya kuteua mwenyekiti wa tume ingawa lazima vyama vya upinzani vishirikishwe kwa uwazi katika suala zima la kuhesabu kura na kutangaza matokeo.
“Hatua hii itasaidia kupunguza malalamiko na pia vyama vya upinzani vitajenga imani na tume ya uchaguzi,” anaeleza Mkapa, ambaye enzi za uhai wake, aliwahi kusuluhisha migogoro ya kisiasa katika nchi za Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, Kenya, Sudan Kusini na Burundi.
Endelea kufuatilia MwanaHALISI Online na MwanaHALISI TV kwa habari zaidi
Leave a comment