DAKTARI Benjamin Mkapa, Rais wa Awamu ya Tatu, amewataka watu wanaoeleza mabaya yake, waseme pia mazuri aliyofanya katika uongozi wake. Anaripoti Mwandishi Wetu, Mwanza … (endelea).
Rais Mkapa ametoa wito huo wakati akizungumza katika uzinduzi wa kitabu cha historia ya maisha yake na uongozi, ‘My Life, My Purpose’, jana tarehe 21 Februari 2020, jijini Mwanza.
Amesema watu wengi hasa wanasiasa, wamekuwa wakimlaumu kutokana na sera alizokuwa anazitekeleza wakati wa uongozi wake, hasa sera ya ubinafsishaji. Pasipo kueleza mazuri yaliyotokana na sera hizo.
“Ukizingatia maelezo kutoka kwa watangulizi walioongea, mtaweza kuonja kidogo faida ya baadhi ya sera nilizotekeleza wakati ule, haya hayasemwi kwenye vyombo vya habari badala yake ni kulaumu tu. Ubinafsishaji ubaya wake na ubaya wa Mzee Mkapa, “ amesema Rais Mkapa.
Rais Mkapa amesema lawama hizo ndizo zilizomsukuma kuandika kitabu hicho na kushauri Watanzania wakisome ili waelewe vyema historia ya uongozi wake.
“Kwa nini niliamua kuandika kitabu hiki ni kwa sababu nalizungumza kwa uwazi na ukweli najua kwamba nalaumiwa sana katika jamii hasa wanasiasa kwa mengi hususan kutokana na sera nilizotekeleza katika uongozi wangu. Nalaumiwa na kusemwa kwamba ni mtu jeuri sana, najiona mimi, msome hiki kitabu na muone kama mimi ni mjeuri kweli,” ameshauri Rais Mkapa.
Leave a comment