RAIS John Magufuli amesema, yeye ni mpangaji wa muda pale Ikulu, na kwamba watendaji kata na Watanzania ndio wanaoamua nani awe mpangaji wa jengo hilo. Anaripoti Regina Mkonde…(endelea).
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo tarehe 2 Septemba 2019, wakati akizungumza na Watendaji wa Kata nchini waliokutana Ikulu, Dar es Salaam.
Kiongozi huyo wa nchi ameeleza, hawezi akawa na kiburi kwa kuwa Ikulu wamekaa watu wengi ikiwemo viongozi wa Kijerumani, Waingereza na hata watangulizi wake.
Viongozi waliomtanguliwa ni Mwl. Mwalimu Julius Nyerere, Alhaj Al Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete.
“Narudia kusema hapa ni kwenu, mimi ni mpangaji tu hapa Ikulu kwa muda, lakini mnaoamuaga nani aende Ikulu ni ninyi na Watanzania, kwa hiyo kamwe siwezi nikafika hapa nikajiona kiburi, hapa wamekaa mpaka Wajerumani hilo jengo limejengwa na Wajeruman.
“Na mimi nitakaa nitaondoka atakuja mwingine, kwa hiyo Ikulu ni mahali pa Watanzania ndio maana sikusita kuwaita hapa,” amesema Rais Magufuli.
Aidha, Rais Magufuli amewataka watendaji kata nchini kutowaogopa viongozi wa serikali na watumishi wa umma wanaofanya makosa katika maeneo yao ya utawala.
“Ninyi si watu wadogo, inawezekana mkawa na maumbo madogo lakini ninyi si watu wa kudharauliwa, wanaweza wakawazidi mshahara lakini ninyi kamwe msidharaulike, na ninyi msitangulize kujidharau, sababu wakati mwingine ninyi mnajidharau,” amesema.
Rais Magufuli amewata watendaji hao kutoa maagizo ya kiutendaji kwa viongozi na watumishi wa umma waliowaizidi cheo.
“usiogope kumlima na kumuandikia mapendekezo ‘recommendation’ hata kama anakuzidi cheo, kwamba katika kata hii ninamuona mtumishi huyu anaenda kinyume na maadili ya kazi zake, na ukimuona ni mkubwa sana ilimradi usimuonee piga nakala hata kwangu,” amesema Rais Magufuli na kuongeza.
“Lazima watu tujifunze kuogopana, kila siku wanapigana kwenye baa iliyo katika kata yako mpaka mwenye baa anafunga baa yake, kwa sababu ya mkubwa fulani unaacha kumripoti sababu ukiripoti waliochini yako watakusumbua, charaza kalamu yako na ndio maana watendaji wa kata wote wanajua kusoma na kuandika na wanasaini zao.”
Leave a comment