RAIS John Magufuli amewataka Watanzania kujihadhari na ugonjwa unaosababishwa na virusi vya corona (COVID-19). Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Ametoa wito huo leo tarehe 21 Februari 2021, wakati akishiriki ibada ya Misa Takatifu ya Dominika ya Kwanza ya Kwaresma katika Parokia ya Mtakatifu Petro, Oysterbay jijini Dar es Salaam.
Pamoja na kumuomba Mungu kuiepusha nchi na corona, Rais Magufuli amewataka Watanzania kuchukua tahadhari kama inavyoelezwa na wataalam wa afya.
Akizungumza kwenye kanisa hilo, amewashukuru Watanzania kupitia madhehebu yao ya dini, kuitikia wito wa maombi na kufung ili Mungu aepushe ugonjwa wa corona.
Taarifa ya Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu imeeleza, Rais Magufuli ameshauri Wakristo ambao wapo katika kipindi cha Kwaresma na Waislamu ambao wanakaribia kuingia katika kipindi cha mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, waendelee kumuomba Mungu.
“Kwani pamoja na jitihada za kibinadamu za kukabiliana na ugonjwa huo, Mungu ndiye muweza wa yote na husimama kwa kila jambo.”
Kwenye taarifa hiyo, amefafanua kuwa serikali haijazuia matumizi ya barakoa katika kujikinga na virusi vya corona.
“Watanzania wachukue tahadhari kwa kutumia barakoa zinazotengezwa hapa nchini zikiwemo za Bodi ya Dawa (MSD) au zinazotengezwa na Watanzania wenyewe.
“Ni kwa kuwa barakoa zinazoingizwa kutoka nje ya nchi, zina mashaka ya kuwa sio salama,” amesema Rais Magufuli.
Pia amesisitiza kutumia njia za asili za kukabiliana na magonjwa ya kupumua ukiwemo ugonjwa huo (corona).
Ametaja njia hizo kuwa ni pamoja na kujifukiza (kupiga nyungu).
Rais Magufuli amewataka Watanzania kuondoa hofu anayosema inayopandikizwa na kwamba, ina madhara zaidi.
Amesisitiza kumtanguliza Mungu kwa kuwa njia za kujikinga kwa barakoa, kutogusana na kutokaribiana.
“Pamoja na kujifungia majumbani, vimeonekana kutokuwa suluhisho la uhakika kwani mataifa yanayofanya hivyo, watu wake wanapoteza maisha kwa maelfu ikilinganishwa na hapa Tanzania,” amesema.
Leave a comment