RAIS John Magufuli amewaweka mtegoni Wakuu wa Wilaya na Mikoa walioko katika maeneo yenye migogoro sugu ya ardhi, akiwataka kusema iwapo wameshindwa kuitatua migogoro hiyo ili awateue wengine. Anaripoti Regina Kelvin … (endelea).
Rais Magufuli ametoa kauli hiyo leo tarehe 6 Septemba, 2018 wakati akizungumza na wananchi wa Butiama katika hafla ya uwekaji jiwe la msingi la mradi wa ujenzi wa barabara ya makutano ya Nyamuswa-Sanzate-Nata na Ikoma Gate katika sehemu ya makutano ya Sanzate, iliyofanyika Butiama mkoani Mara.
“….Ukikaa mahali kukiwa na migogoro mjue mmeshindwa kutawala, kuna polisi, kuna sheria ya ardhi na ya vijiji, mna madaraka haiwezekani mkakaa mahali kukawa na migogoro mpaka watu wanashindwa kulima na mvua imenyesha. Kama mmeshindwa kutatua migogoro mseme mmeshindwa nilete wengine. Haiwezekani nchi hii watu wanagombea mipaka tena wote ni watanzania wanazungumzia lugha moja,” amesema.
Rais Magufuli amesema kuwa, ni aibu kwaTaifa lililosifika kwa kutokuwa na migogoro ya ardhi kutokana na hekima za Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, kuwa na migogoro hasa katika mkoa wa Mara aliotoka mwasisi huyo wa Taifa.
“Baba wa taifa alizuia migogoro mingi, taifa hili lilisifika kwa kutokuwa na migogoro mingi kutokana na hekima ya baba wa taifa, Ninawaomba msimwaibishe baba wa taifa kwa kuwa na migogoro mingi.” Amesema na kuongeza.
“Mkoa huu migogoro ya ardhi imekuwa ni tatizo, migogoro kati ya vijiji na vijiji na mtu na mtu. Tusije kuwa na migogoro wakati tunaweza kuimaliza wenyewe. Haiwezekani kuwe na vijiji vina mgogoro ndani ya mkoa mmoja, inabidi tuimalize wenyewe.
“Tusiliingize taifa kwenye ,migogoro hiyo. Ninawaomba wakazi wa Butiama, Bunda na maeneo jirani msigombane, msisubiri viongozi wa nchi wa wilaya au mikoa watatulie migogoro yenu.”
Leave a comment