RAIS John Magufuli ametuma pole kwa Waislam nchini kutokana na kifo cha aliyekuwa Sheikh wa Mkoa wa Mwanza, Salum Hassan Fereji. Anaripoti Yusuph Katimba…(endelea).
Sheikh Fereji alifariki dunia usiku wa kuamkia Julai 28 alipokuwa amelazwa katika Hospitali ya Rufaa ya Bugando, Mwanza kutokana na kusumnuliwa na ugonjwa wa kisukari na shinikizo la damu
Hayati Sheikh Fereji alifanyiwa ibada ya swala Julai 29, 2018 katika msikiti wa Raudhwa uliopo Mtaa wa Lumumba, Mwanza na kuzikwa siku hiyo hiyo.
Mazishi hayo yalihudhuriwa na viongozi mbalimbali wa serikali na dini akiwemo Mufti wa Tanzania, Aboubakary Zubeir.
Salamu za pole za Rais Magufuli pia alizielekeza kwa Mufti Zubeir ambapo amesema, anamkumbuka Sheikh Fereji kwa ucha Mungu wake, ukarimu, upendo kwa wananchi na namna alivyokuwa akiunga mkono juhudi za kudumisha amani na kusukuma mbele maendeleo.
“Nimesikitishwa sana na kifo cha Sheikh Fereji, nilipokuwa nikienda Mwanza alikuwa miongoni mwa viongozi wa dini waliokuja kunipokea.
“Amekuwa akifanya kazi ya Mwenyezi Mungu kwa mapenzi makubwa na nchi yake, pole sana Mufti wa Tanzania na nakuomba unifikishie salamu zangu za pole kwa familia yake, Waislamu wote wa Mkoa wa Mwanza na nchi nzima pamoja na wote walioguswa na msiba huu,” amesema Rais Magufuli.
Leave a comment