RAIS wa Tanzania,John Pombe Magufuli amefanya uteuzi wa Wakuu wa Mkoa (RC) wawili na Wilaya (DC) tisa. Anaripoti Mwandishi Wetu, Dar es Salaam…(endelea).
Taarifa iliyotolewa leo Ijumaa tarehe 3 Julai na Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais Ikulu imesema uteuzi wa viongozi hao umeanza leo.
Msigwa amesema, MRais Magufuli amemteua Dk. Philemon Sengati kuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora.
Kabla ya uteuzi huo, Dk. Sengati alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Magu mkoani Mwanza na anachukua nafasi Aggrey Mwanri ‘mzee wa sukuka ndani’ ambaye amestaafu.
Pili, Rais Magufuli amemteua Thobias Andengenye (aliyewahi kuwa Kamishna Jenerali wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji) kuwa Mkuu wa Mkoa wa Kigoma.
Andengenye anachukua nafasi ya Brigedia Jenerali Mstaafu Emmanuel Maganga ambaye amestaafu.
Wakuu wa Wilaya walioteuliwa, Wakati huo huo, Kwanza, Rais Magufuli amemteua Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Magereza (SACP) Ismail Twahir Mlawa kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kilombero mkoani Morogoro.
Kabla ya uteuzi huo, Mlawa alikuwa Mkuu wa Magereza wa Mkoa wa Morogoro na anachukua nafasi ya James Mugendi Ihunyo ambaye amestaafu.
Pili, Rais Magufuli amemteua Jamila Yusuf kuwa Mkuu wa Wilaya ya Mpanda Mkoa wa Katavi.
Kabla ya uteuzi huo, Jamila Yusuf alikuwa Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dodoma na anachukua nafasi ya Lilian Charles Matinga ambaye amestaafu.
Tatu, Rais Magufuli amemteua Mhandisi Martine Ntemo kuwa Mkuu wa Wilaya ya Kibaha Mkoa wa Pwani.
Kabla ya uteuzi huo, Mhandisi Ntemo alikuwa Mhandisi katika Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano na anachukua nafasi ya Asumpter Nshunju Mshama ambaye amestaafu.
Nne, Rais Magufuli amemteua, Salum Kali kuwa Mkuu wa Wilaya ya Magu Mkoa wa Mwanza.
Kabla ya uteuzi huo, Kali alikuwa Katibu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Mwanza na anachukua nafasi ya Dk. Philemon Sengati ambaye ameteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Tabora.
Tano, Rais Magufuli amemteua Wilson Samwel Shimo kuwa Mkuu wa Wilaya ya Nyang’wale Mkoa wa Geita.
Kabla ya uteuzi huo, Shimo alikuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Singida.
Sita, Rais Magufuli amemteua Kanali Mathias Kahabi kuwa Mkuu wa Wilaya ya Biharamulo Mkoa wa Kagera.
Kanali Kahabi anachukua nafasi ya Saada Malunde ambaye amestaafu.
Saba, Rais Magufuli amemteua Abbas Kayanda kuwa Mkuu wa Wilaya ya Karatu Mkoa wa Arusha.
Kabla ya uteuzi huo, Kayanda alikuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Karatu na anachukua nafasi ya Theresia Jonathan Mahongo ambaye amestaafu.
Nane, Rais Magufuli amemteua Lazaro Jacob Twange kuwa Mkuu wa Wilaya ya Babati Mkoa wa Manyara.
Bwana Twange anachukua nafasi ya Elizabeth Simon Kitundu ambaye amestaafu.
Tisa, Rais Magufuli amemteua Toba Alnason Nguvila kuwa Mkuu wa Wilaya ya Handeni
Kabla ya uteuzi huo, Nguvila alikuwa Katibu Tawala wa Wilaya ya Longido Mkoani Arusha na anachukua nafasi ya Godwin Gondwe ambaye amehamishwa kituo cha kazi na kuwa Mkuu wa Wilaya ya Temeke Mkoani Dar es Salaam.
Godwin Gondwe anachukua nafasi ya Felix Jackson Lyaniva ambaye amestaafu.
“Uteuzi wa viongozi hao umeanza leo tarehe 03 Julai, 2020 na wateule wote wanatakiwa kuwepo Ikulu, Chamwino Mkoani Dodoma tarehe 06 Julai, 2020 saa 4:00 asubuhi,” amesema Msigwa.
Leave a comment