RAIS John Magufuli amesema, amemfukuza kazi Mrisho Gambo, aliyekuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha na wenzake wawili, kutokana na kutotekeleza maagizo yake. Anaripoti Regina Mkonde, Dar es Salaam … (endelea).
Tarehe 19 Juni 2020, Rais Magufuli alitengua uteuzi wa Gambo, Gabriel Daqarro ambaye alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Arusha na Dk. Maulid Madeni, aliyekuwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha.
Rais Magufuli ametaja sababu hizo leo Jumatatu tarehe 22 Juni 2020, wakati akiwaapisha viongozi wapya aliowateua kwa ajili ya kujaza nafasi zao.
Rais Magufuli amesema, ametengua uteuzi wa viongozi hao kutokana na kutofurahishwa na mienendo yao, ikiwemo kugombana kwa takribani miaka miwili.
“Mimi saa nyingine nasikitikaga sana unapoona watu uliowateua na ukawaapisha na kuwaamini kwa niaba ya Watanzania, wanapoenda kule hawafanyi kadri ya viapo, mtakumbuka hivi karibuni nilitengua uteuzi wa wote kuanzia, sababu katika kipindi cha miaka mwili walikuwa wanagombana tu,” amesema Rais Magufuli na kuongeza:
“Kila mmoja ni bosi anatengeneza mizengwe kwa mwenzake sikufurahishwa, walifanya kazi zao lakini waliniudhi wao kutoshirikiana na kufanya yale ambayo nimewaagiza, sasa nimewateuwa ninyi sitaki yakajitokeze hayo.”
Rais Magufuli amewaagiza viongozi wapya aliowaapisha kujaza nafasi zao, kwenda kufanya kazi kwa mujibu wa viapo vyao, ili changamoto zilizojitokeza zisijirudie tena.
Viongozi aliowaapisha ni, Iddi Kimanta, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Kena Kihongosi, Mkuu wa Wilaya ya Arusha na Dk. John Pima, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha.
Leave a comment