SERIKALI inayoongozwa na Rais John Magufuli imepongezwa kwa kufanya vizuri katika utekelezaji wa kutoa na kuchukua hatua hasa katika magonjwa ya mlipuko. Anaandika Khalifa Abdallah… (endelea).
Pongezi hizo zimetolewa na Kituo cha Kimataifa cha Kufuatilia, Kutathimini, Kutoa Taarifa na Kuchukua Hatua (CDC) kilichopo nchini Marekani.
Hayo yamesemwa na Ummy Mwalimu ambaye ni Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto wakati wa kikao cha kuangalia hali ya utendaji katika sekta ya afya nchini.
“Wenzetu wa CDC kutoka Marekani wanatusaidia kujenga uwezo wa kufuatilia, kutoa taarifa na kuchukua hatua juu ya magonjwa ya mlipuko kama vile Ebola na Kipindupindu na wameridhika kwa utendaji wetu hapa nchini,” amesema Waziri Ummy.
Amesema kuwa, Tanzania imeimarika katika kufanya uchunguzi, kutathimini, kutoa taarifa na kuchukua hatua juu ya magonjwa mbalimbali.
Mbali na hayo amesema kuwa, magonjwa hayana mipaka hivyo ni lazima kuwa waangalifu na kuchukua hatua mda wote kwa kujenga mifumo imara ya ufuatiliaji.
Inmi Petterson, Kaimu Balozi wa Marekani nchini amesema kuwa, wamefurahishwa na kazi ya wataalamu wa afya waliowekwa hapa nchini katika kupambana na magonjwa na kuahidi kuongeza nguvu kubwa ikiwemo vitendea kazi.
Aidha Balozi Inmi amesesema kuwa, Serikali ya Tanzania inatakiwa kushirikiana na wananchi wake katika kupata taarifa sahihi za magonjwa na kujenga nchi yenye wananchi wenye afya bora.
Leave a comment