RAIS John Magufuli ameungana na Watanzania kutoa salamu za rambirambi kwa uongozi wa Kampuni zilizo chini ya Azam Media zinazoongozwa na mwenyekti wake Said Salim Bakhresa, kufuatia vifo vya wafanyakazi wake watano. Anaripoti Regina Mkonde … (endelea).
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa leo tarehe 8 Julai 2019 na Gerson Msigwa, Mkurugenzi wa Mawasiliano ya Rais-Ikulu, Rais Magufuli amempa pole Bakhresa na ndugu wa marehemu wote.
“Nimeshtushwa sana na vifo hivi, nampa pole Mwenyekiti Ndg. Said Salim Bakhresa, ndugu wa marehemu wote, Mtendaji Mkuu, Ndg. Tido Mhando na wafanyakazi wote wa Azam Media Ltd, Waandishi wa habari wote na watu wote walioguswa na vifo hivi,” amesema Rais Magufuli.
Vile vile, Rais Magufuli amewaombea marehemu wapumzike kwa amani na majeruhi wa ajali hiyo wapone haraka ili waweze kuendelea na majukumu yao ya kila siku.
Aidha, Rais Magufuli ametoa wito kwa watumiaji wa barabara hususani madereva kuwa makini na kuzingatia sheria za usalama barabarani ili kuepusha ajali zinazoweza kuepukika.
Wafanyakazi hao wa Azam Media Ltd wamefariki dunia asubuhi ya leo eneo la Kizonzo katikati ya Igunga (Tabora) na Shelui (Singida) katika ajali ambapo basi aina ya Coaster waliokuwa wakisafiria kuelekea Mwanza wakitokea jijini Dar es Salaam, liligongana uso kwa uso na Lori la mizigo lilikuwa linakwenda Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa taarifa ya Msigwa, wafanyakazi hao walikuwa safarini kuelekea kwenye sherehe za uzinduzi wa Hifadhi ya Taifa ya Burigi-Chato kwa ajili ya kurusha matangazo ya moja kwa moja ya sherehe hizo.
Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF) limetuma salamu za rambirambo kwa wafanyakazi wote wa Azam Media Limited kutokana na vifo hivyo.
Taarifa ya Nevile Meena, Katibu wa TEF imeeleza kuwa, ajali hiyo imeacha pigo na simanzi kubwa kwa tasnia ya habari na wanahabari kwa ujumla.
“TEF limepokea kwa mshtuko mkubwa taarifa za ajali ya gari iliyosababisha vifo vya wafanyakazi watano wa Azam Media waliokuwa safarini kuelekea Chato kutekeleza wajibu wao wa kitaaluma. Tunaungana na wanataaluma wote wa tasnia ya habari nchini kuupa pole uongozi, menejimenti na wafanyakazi wa Azam,” imeeleza sehemu ya taarifa ya TEF.
Leave a comment