RAIS John Magufuli ametengua uteuzi wa mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa, Mohamed Maje kuanzia leo kwa kushindwa kutekeleza majukumu yake. Anaripoti Dany Tibason … (endelea).
Akitoa taarifa ya utenguzi huo mjini Dodoma, Katibu Mkuu wa Tamisemi, Alhaji Mussa Iyombe amesema kuwa Maje ameisababishia serikali hasara ikiwemo kushindwa hata kukusanya mapato ya serikali.
Utenguzi wa Maje umetokana na taarifa iliyotolewa na tume iliyoundwa kukagua utendaji wake wa kazi nakubaini kuwa ameshindwa kusimamia na kudhibiti mapato ya halmashauri hali iliyopelekea upotevu wa fedha.
“Hadi kufikia robo tatu ya mwaka wa fedha halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa imekusanya mapato kwa asilimia 24 tu pamoja nakuwa halmashauri hiyo ni kongwe na yenye vyanzo vingi vya mapato,” amesema Iyombe.
Hatua hii imekuja baada ya Mkuu wa mkoa wa Dodoma Dk. Bilineth Mahenge kuagiza kuundwa kwa tume ya mkoa kuchunguza ubadhilifu wa fedha zaidi ya Sh. 500 milioni katika halmashauri ya wilaya ya Mpwapwa pamoja na kubaini sababu za halmashauri hiyo kuwa ya mwisho katika ukusanyaji wa mapato.
Akizungumza katika kikao cha ushauri wa mkoa (RCC) Mahenge alionyesha kusikitishwa na matokeo hayo pamoja na kuwa wilaya Kongwe nayenye vyanzo vingi vya mapato kukusanya asilimia 24 pekee ya mapato hivyo kupelekea kuchukuliwa hatua kwa watendaji wote wanaokwamisha ukusanyaji wa mapato ya ndani.
Hata hivyo Mahenge alisisitiza uadilifu kwa watendaji ikiwa ni pamoja na kupeleka mashine za kukusanyia mapato katika kata.
“Ukusanyaji wa mapato ya ndani ni muhimu sana katika halmashauri kwani ndio hutumika katika shughuli za maendeleo,ukuaji na ustawi wa halmashauri,” amesema Mahenge.
Leave a comment